FAHARI YA MACHO INAPOFILISI DUKA: Mbweni, Maadili na Soko Huria la Unafiki
Kuna msemo wa Kiswahili usemao: “Samaki mkunje angali mbichi.” Lakini sisi tumengoja mpaka samaki awe stockfish wa Norway, kisha tunashangaa kwa nini havunjiki bila nyundo.
Nimeitazama simulizi ya wakaazi wa Mbweni, Zanzibar, wakisimama kidete kupinga baa na kumbi za starehe katika maeneo yao ya makazi. Wakisema wanalinda maadili. Wakisema wanazuia uhalifu. Wakisema wanataka mazingira salama kwa watoto wao. Maneno mazuri. Maneno ya kuvutia. Maneno yanayopata likes na views kwa kasi kuliko sera za ajira.
Lakini kama alivyotuonya Karl Marx, mara nyingi jamii hupenda kushughulika na superstructure—dalili—wakati base ya kiuchumi ndiyo inayozalisha tatizo. Baa siyo mzizi; ni tawi. Kumbi za starehe si chanzo; ni kivuli cha mti uliopandwa zamani kwa mbolea ya utalii, soko huria na uchumi wa huduma.
Tuliposema “karibuni wageni”, tulimaanisha wageni wa aina gani? Tulipofungua milango kwa jina la uwekezaji, tulifikiri mitaji huja na tasbihi? Au tulidhani fedha huingia bila falsafa yake?
Max Weber aliwahi kueleza kuhusu “roho ya ubepari” – ile ari ya kimaslahi inayovaa suti ya maadili lakini moyoni ina hesabu za faida. Leo tunashuhudia roho hiyo ikitembea Mbweni kwa jina la “burudani”, “ajira kwa vijana”, “ukuaji wa uchumi”. Na sasa, wale wale waliopiga makofi wakati majengo yanapanda, wanashika mawe majengo yanapotoa kelele.
Ni vigumu kula keki na kuendelea kuimiliki.
Jamii yetu ilijenga uchumi wa utalii kwa mikono yake miwili. Ikaupa kipaumbele. Ikaufanya uti wa mgongo. Leo tunasema uti huo una maumivu ya maadili. Lakini uti hauwezi kuugua bila mwili mzima kushiriki. Kama alivyosema Émile Durkheim, jamii inapopoteza mwelekeo wa pamoja huingia katika hali ya anomie—mkanganyiko wa maadili. Hapa ndipo tulipo: tunataka soko huria, lakini kwa masharti ya madrasa; tunataka dola ya kisasa, lakini kwa maadili ya kijiji kisichobadilika.
Na tusijidanganye—tatizo si pombe pekee. Tatizo ni mabadiliko yasiyosimamiwa. Ni mipango miji iliyoachwa mikononi mwa tamaa. Ni pengo la ajira linalowasukuma vijana kwenye “uchumi wa usiku”. Ni magari yanayotumika kama vyumba vya siri kwa sababu nyumba hazina faragha na mazungumzo ya ngono ni mwiko mchana lakini biashara usiku.
Tunahukumu matokeo, tunalea sababu.
Wakaazi wa Mbweni wana haki ya kuhoji. Lakini pia lazima tujiulize: Je, tulichelewa? Je, tulipoona mchicha unaota pembeni ya nyumba tulidhani ni mboga ya leo, tusijue kesho utakuwa mbuyu? Tulipoona vibali vinatolewa, tulinyamaza kwa sababu “mwenye nacho” alikuwa amenyoosha mkono?
Hapa ndipo kejeli inapoanza kujicheka yenyewe.
Kwa miaka mingi, Unguja na Pemba vilijulikana kwa utulivu, kwa ustaarabu, kwa elimu na kwa ukarimu. Lakini pia vilijulikana kwa ukimya wa kukubali. Ulikuwa ukimya wa busara au wa woga? Ulikuwa uvumilivu au uzembe wa kimfumo?
Antonio Gramsci alizungumza juu ya hegemony—namna tabaka tawala linavyofanya fikra zake zionekane kama fikra za wote. Leo ukisema “hii ni haki ya kikatiba ya kufanya biashara”, mjadala unafungwa. Ukisema “haya ni maadili ya jamii”, mjadala mwingine unafungwa. Haki dhidi ya maadili. Uchumi dhidi ya utamaduni. Njia panda.
Na njia panda haichagui mwenye haraka.
Wengine wanasema haya ni mabadiliko ya wakati. Sawa. Lakini si kila kinachoitwa maendeleo ni ustaarabu. Na si kila kinachoitwa maadili ni suluhisho. Kijana akija nyumbani uchi kutafuta hifadhi, je, ni “kwenda na wakati” au ni dalili ya mfumo uliomwacha njiani? Swali si la kejeli tu; ni la sera.
Tatizo la Mbweni si Mbweni peke yake. Ni kioo. Leo ni kule, kesho ni Kinuni, keshokutwa ni Nyarugusu. Leo tunapinga baa; kesho tutapinga ajira zinazotokana na baa. Leo tunasema ondokeni; kesho tutasema vijana hawana kazi.
Hii ndiyo paradox ya jamii inayotaka matokeo ya ubepari bila athari zake.
Kuachia yaendelee si busara. Kuyaondoa kwa ghafla ni hatari. Suluhisho si kufunga milango yote, wala si kuacha wazi bila bawaba. Suluhisho ni sera makini, upangaji miji, udhibiti, na zaidi ya yote—uamuzi wa pamoja unaochelewa lakini si “too little too late”.
La sivyo, fahari ya macho itaendelea kufilisi duka la maadili. Tutabaki na mabango ya “mazingira salama” huku usiku ukiendelea kuuza tiketi.
Mimi si mhubiri, wala si mpiga debe wa starehe. Ninasema tu: tusipende kupambana na kivuli cha mti tulioupanda wenyewe. Kama mzizi ni mkubwa kama mbuyu, basi hatuwezi kuuangusha kwa fimbo ya mkutano mmoja wa wananchi.
Tunahitaji shoka la sera, si miayo ya hasira.
Na kama mkono wa kuume una nguvu, basi utumike kwa hekima, si kwa jazba. La sivyo tutajikuta tunasulubiwa na maamuzi yetu wenyewe, tukilia juu ya paa tulilojenga kwa mikopo ya sifa na kulipa kwa riba ya maadili.
Mungu atufanyie wepesi—lakini kabla ya wepesi wa mbinguni, tujifanyie ujasiri wa duniani.
Lakini kabla hatujamaliza kwa dua, labda tuanze na maswali—kwa sababu jamii inayokimbia maswali huishia kuabudu majibu mepesi.
Je, maadili ni kitu kinacholindwa kwa kufunga mlango wa baa, au ni kitu kinachojengwa kwa kufungua mlango wa fursa?
Je, tunapopiga vita pombe, tunapiga vita kemikali au tunapiga vita upweke, ukosefu wa ajira na kukata tamaa?
Je, soko huria linaweza kuvaa kanzu ya utamaduni bila kuacha harufu ya faida?
Je, haki ya kikatiba ya kufanya biashara ina mipaka pale inapoanza kugusa usingizi wa mtoto wa jirani, au haki huwa haina majirani?
Je, jamii inaweza kudai usafi wa maadili huku ikiishi kwa kodi na ajira zinazotokana na kile kile inachokilaani?
Je, tulipofungua milango ya utalii tulijua kwamba wageni huja na mizigo yao ya fikra, au tulidhani mizigo yao huishia uwanja wa ndege?
Je, tunachokipinga leo ni baa, au ni kioo kinachotuonyesha sura yetu tuliyoisahau?
Je, maendeleo ni nini—idadi ya majengo au ubora wa roho?
Na kama maendeleo yanapimwa kwa fedha, je, maadili yanapimwa kwa nini?
Je, tunaposema “zamani haikuwa hivi” tunamaanisha zamani kulikuwa na usafi, au zamani kulikuwa na siri?
Je, kizazi cha leo kimeharibika, au kimeacha kuogopa kusema kile kilichokuwa kikifanyika gizani?
Je, tatizo ni kelele za muziki, au ukimya wa sera?
Je, tukifunga baa zote, tutajenga viwanda?
Na tusipojenga viwanda, tutafunga nini tena ili kujisitiri?
Je, jamii inaweza kubaki kisiwa cha maadili katikati ya bahari ya utandawazi, bila kuogelea wala kuzama?
Na mwisho kabisa—
Je, tunataka kweli suluhisho, au tunataka tu adui wa kumlaumu?
Kwa sababu huenda tatizo si Mbweni.
Huenda tatizo ni sisi.
Na huenda suluhisho si kufukuza kivuli, bali kukubali kwamba mwanga tunaoutafuta lazima uanze ndani yetu.
Wasalam Ramadhan Maqbool.