Tuesday 25 November 2014

MaalimSeif awasili Mkoani Mtwara

  1. Maalim Seif akiwasalimia na Wazee  wa Mkoa wa Mtwara wakati alipowasili mkoani huo kwa ziara yake.jana.

Na.Khamis Haji, OMKR
Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi CUF, Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad amepata mapokezi makubwa ya wanachama wa chama hicho na wananchi alipowasili mkoani Mtwara kwa ziara ya kichama katika mkoa huo pamoja na mkoa wa Ruvuma.
Mara baada ya kuwasili uwanja wa ndege wa Mtwara Maalim Seif ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar alipokelewa kwa ngoma na vijana wa mapikipiki na gari yaliyokuwa na bendera za CUF na kuusindikiza msafara wake katika mitaa mbali mbali ya mji wa Mtwara. Akimkaribisha katika mkoa huo, Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Mtwara ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Tandahimba, Ponsiano Nyami alimweleza Maalim Seif kuwa sasa yuko huru kufanya mikutano ya hadhara na shughuli zote za kisiasa kutokana na hali ya mkoa huo kuwa tulivu. “Karibu sana Mtwara na unaruhusika kufanya mikutano ya hadhara. Pale nyuma ulipotaka kuja nilikuzuia kwa sababu hali haikuruhusu kutokana na kukosekana amani na utulivu”, alisema Mkuu huyo wa Wilaya alipokuwa uwanja wa ndege wa Mtwara.

Wanachama wa CUF na wananchi hao walimzuia Maalim Seif kwa muda nje ya uwanja ili apate kuwasalimia na ndipo alipokwenda kusimama na kuwasalimia kwa salamu za CUF ‘Haki’ nao wakipaza sauti kuitikia salamu hizo.Baadaye misafara ya magari, pikipiki na baiskeli zilifuatana na msafara wake wakisindikizwa na gari ya Polisi ya kikosi cha kutuliza ghasia yenye namba PT 2119 hadi hotelini alipofikia. Baadhi ya wafuasi hao walikuwa wakisema ‘bado hatujasahau’ na wengine kuimba ‘kidume’ ‘kidume’.Maalima Seif ambaye amefuatana na Naibu Mkurugenzi wa Habari, Uenezi na Mawasiliano ya Umma wa CUF, Abdul Kambaya katika ziara hiyo atahutubia mikutano kadhaa ya hadhara katika Wilaya mbali mbali za Mtwara na baadaye Ruvuma ambapo pia atafanya mikutano ya ndani kwa viongozi wa chama hicho.    Ziara ya Maalim Seif inakuja baada ya takriban miezi mitano iliyopita kuzuwiwa kuingia mkoani Mtwara, baada ya kuelezwa na viongozi wa mkoa huo kuwa hali ya usalama hairusu kufanya shughuli za kisiasa. 

No comments: