Sunday 4 October 2015

Kingunge ajitoa rasmi CCM

 
Mwanasiasa mkongwe ambaye ni kada maarufu wa chama cha CCM Ndugu Kingunge Ngombale Mwiru ametangaza rasmi kujivua uanachama wa chama hicho cha siasa na amesema sababu kubwa ni kutokana na kutoridhishwa na mwenendo wa chama hicho kwa sasa.Amesema hatojiunga na chama kingine cha siasa ila anaamini vijana, kinamama, na watanzania wanahitaji mabadiliko na yeye yuko upande wa mabadiliko.



MANENO YA MZEE WETU KINGUNGE NGUMBARU MWIRU



Anasema kamati kuu haiwezi kusema watu watano au sita ni hawa bila kuwasikiliza, kilichotokea mwaka huu ni tofauti kabisa kilichotokea mwaka 1995, safari mwenyekiti ni Jakaya Kikwete, kilichotokea ni jambo kubwa katika historia yetu na mimi katika historia yangu pale ambapo naona kwamba katiba inavunjwa nimekuwa na tabia ya kusema waziwazi na kuwaambia wenzangu si sawa.


Mwaka 1972 nikiwa mkuu wa mkoa Simiyu, kulikuwa na Bunge Dar es Salaam, nikakuta kuna mswada wa kurekebisha katika kuhusiana na swala la wakuu wa mikoa. Mchango wangu uliibua hisia kali na kumwambia mwenyekiti muswada aurudishe maana hatuukubali, kwa upande wa watu walipo serikalini walisema ndio na wabunge wa kuchaguliwa walisema hapana.


Ilipofika zamu yangu nikasema sina upande, wabunge walifurahi sana. Kura zilipohesabiwa serikali ilishindwa kwa mara ya kwanza katika mfumo wa serikali ya chama kimoja. Mzee Kawawa aliniita akasema wewe ni mwenzetu lakini umetuacha, Rais atakubadilisha kazi.


Nilipoitwa na mwalimu nilimueleza kwa nini nilikataa na akasema ningekuwa katika nafasi yako ningepinga lakini mimi ndio naongoza nchi lakini usiwe na wasiwasi. Tukakubaliana na siku ya pili nikatangazwa nimeachishwa uwaziri. Nilifanya uamuzi ule nikijua kabisa naweza kupoteza kazi lakini kwenye masula ya kimsingi huwa sitetereki.


Mimi sikubaliani na mambo yaliyotokea tarehe kumi na kumi na moja Dodoma, kilichotokea ni kuwadhalilisha wagombea wenye haki, kamati kuu ingeweza kuwahoji na kuamua. Hili halikfanyika. wadhalilishwa, wamezungushwa mikoa 15 kwa gharama zao na kuishia mlangoni mwa kamati kuu.


CCM inaamini binadamu wote ni sawa na kila mtu anastahili heshma ya kutambuliwa utu wake, kuwazungusha alafu nyinyi mmefunga mlango, si kuwadhalilisha? Katika nchi yetu hao waliodhalilishwa wamenyamaza moja kwa moja isipokuwa Mwandosya, aliinuka na kusema kwamba kweli wamedhalilishwa na kadhalika.


Nawapongeza Kimbisa, Sophia na Nchimbi kwa kueleza yaliyotokea kamati kuu, tuliingia chama hiki si kwa ajili ya kutafuta cheo na wengine tuliacha kazi kwa mkoloni. Tulitafuta chombo cha ukombozi kwa watanzania na waafrika.


Kwa kuwa uongozi wa sasa wa chama cha mapinduzi kufanya yale wanayotaka wao kwa maslahi ambayo sina hakika ni ya nani, vijana wanatumiwa kudhalilisha watu wazima, watu wanaajiriwa kutukana tu watu, mimi nasema sikubaliani na hiko sio chama tulichoshirikiana kukijenga.


Mimi kuanzia leo naachana na chama cha mapinduzi kwa sababu siwezi kuhimili chama kinachoendeshwa bila kuheshimu katiba kwa sababu katiba ndio inayotuunganisha sisi sote. Sasa nasema kuanzia sasa najitoa chama cha mapinduzi, najua uamuzi wangu utasumbua baadhi ya rafiki zangu, makada wenzangu na wazee wenzangu hata vijana lakini ni uamuzi ambao lazima niufanye kwa sababu vinginevyo mimi nitajisaliti mwenyewe.


Nimehusika kuweka misingi ya chama chetu, ndani ya chama chetu kumekuwa na demokrasia halafu wakuu wanakwenda kutangaza kwenye majukwaa hakukuwa na tatizo lolote, mambo yote yalikuwa sawasawa.


Sikusudii kujiunga na chama kingine chochote na nina sababu, mimi nimekuwa mwanaharakati wa TANU na CCM kwa muda wa miaka 61, nadhani miaka 61 inatosha mimi kuwa mwanaharakati.


Tatu mimi ni raia tena raia huru wa jamuhuri ya muungano wa Tanzania, nna haki zangu za kisisasa na kijamii hivyo nitaendelea misimamo yangu.


Katika hali ya sasa ina makundi mawili, moja linasema kidumu chama tawala maana yake hakuna mabadiliko. Kundi jingine linasema linataka mabadiliko katika nchi yetu, sitaki kusema kundi lipi kubwa lakini nasema hali iko hivyo, kwa jinsi nnavyotazama vijana wanataka mabadiliko ukiondoa vijana wangu wa UVCCM, kina mama walio wengi wanataka mabadiliko, wafanyakazi wakulima, wafugaji, wavuvi, wachimba migodi wadogowadogo najua wengi wao wanataka mabadiliko, wanafunzi hasa wa sekondari ya juu, wa vyuo na vyo vikuu na wasomi wa nchii walio wengi wanataka mabadiliko.


Nilisema siku moja nilipoulizwa nani unamuona anafaa kugombea Urais, niliwaambia kwamba mimi nitamuunga mkono yule ambae ziko dalili zote wananchi wanasema ndie anaefaa. Pia nilisema nilipokuwa na ndugu Lowassa Arusha, Mwalimu alisema ulizeni wananchi wanasema nini?


Katika hili swala la mabadiliko mimi niko upande wa mabadiliko tena mimi nasema wamechelewa, walio wengi wanataka mabadiliko. Mimi nasema niko upande wa mabadiliko kwa sababu ya wale. Katika historia yetu katika TANU na Afro shirazi sisi tulikuwa upande wa mabadiliko.


Tuliungana na hio ilikuwa mabadiliko, mwaka 77 tuliua Afro Shirazi, tuliua TANU na kufanya mabadiliko.

Baada ya kukaa madaraki miaka mingi hatuwezi kuleta jipya pamoja na ahadi za Magufuli, nusu karne ni muda mrefu sana, pumzi, kuongoza nchi na kama kupanda mlima, unafika mahala pumzi zinakwisha, huwezi kuendelea mbele na ukitaka kuendelea wananchi wanabaki palepale walipo.


Tatizo la wananchi ni uchumi, ajira, sasa umasikini unaondolewa na uchumi imara.


Mkapa alitufanyia kazi nzuri kwa kututoa kwenye ukuaji wa asilimia 3 mpaka 4, wakati anakabidhi madaraka ulikuwa unakuwa kwa 7%. Kikwete amepokea madaraka unakuwa kwa 7%, sasa miaka kumi baadae uchumi unakuwa kwa 7%. Maana yake miaka kumi hii tumepiga maktaimu, tumebaki palepale maana yake ni kurudi nyuma.


Idadi ya watu imeongezeka, midomo imeongeza, miguu imeongezeka lakini ukuaji uko palepale, bei ya sukari kwa mfano ni ya kuruka, bei ya sukari Mkapa aliacha 600 sasa inaenda 2000. Nini! Pumzi. Kwenda kwenye maisha bora kunataka pumzi.


Tulianza na maisha bora kwa kila mtanzania lakini sasa hatusemi tena habari hizo, mabadiliko ni muhimu kwelikweli, tupate pumzi mpya. Mnataka mbaki nyinyi tu, nyinyi pumzi imekwisha. Chama kifutike? Hapana lakini kiwekwe benchi kidogo kijitafakari.


Kama hamjadili mambo mtapata wapi mawazo ya kwenda mbele, lazima ukuaji wa uchumi wa nchi angalau ufike 10%. 7% mpaka 10% si mbali lakini miaka kumi tuko palepale. Wachina wamekuwa wakikuza uchumi wao mpaka asilimia 15 na zaidi, na sisi hapa baadhi yetu kama watu watakuwa wanyenyekevu kupata mawazo ya wenzao tutapiga hatua.


Mimi nimekuwa mwenyekiti wa ilani zote za uchaguzi kasoro moja tangu mwaka 90, tatizo la ajiri kwa vijana linaonekana kana kwamba halitatuliki wakati linatatulika, kujiajiri na kutoa mitaji. Wanaotaka kujidanganya kwamba wataleta mabadiliko haya!


Lakini tunaotaka kwenda mbele, kung'ang'ania kwamba lazima wao wawe madarakani mtakuja kujilaumu wenyewe siku moja. Asanteni sana kwa kunisikiliza.


SWALI(Mayage): Kama CCM mngemteua Lowassa, ungayasema hayo ya kusema unataka mabadiliko?


Jibu: Mimi wakati wote nimekuwa nina matumaini kwamba ndani ya CCM tunaweza kupata watu wanaoweza kubadili hali ndio maana niliamua kupambana ndani ya chama changu tukaenda mbio kuliko hivi ili hali ya wananchi ibadilike. Mimi nikamuona Edward Lowassa kwa jinsi ninavyomjua, si mtu mgeni katika nchi hii, nikasema tukimpata nchi itakwenda mbio zaidi.


Niliwahi kuzungumza kwanini nilisimama sambamba na Edward Lowassa kule Arusha, nikasema Edward ana sifa kuliko wengi niliowaona, kiongozi lazima akubalike na watu na hii ni principle ya watu tangu TANU, Lowassa anakubalika pamoja kupakaziwa mambo ya ajabu.


Matangazo ya ITV yameishia hapa, maswali yanaendelea.

No comments: