Mbali na kutoshiriki uchaguzi wa marudio unaosimamiwa na ZEC, pia CUF inawataka wanachama, wafuasi wake na wananchi wote kutoshiriki katika uchaguzi wa marudio katika Jimbo la Kijitoupele unaosimamiwa na Tume ya Tiafa ya Uchaguzi (NEC). CUF inawataka wananchi kususia uchaguzi huo kwa sababu kwa Zanzibar ni ZEC ndio hufanya kazi kama wakala wa NEC, hivyo hakuna haki itakayotendeka
katika uchaguzi huo.
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI    18 Machi, 2016
Siku ya Jumapili, tarehe 20 Machi 2016, Zanzibar itashuhudia, kwa mara nyingine tena, ubakwaji wa demokrasia kwa kufanyika kile kinachoitwa Uchaguzi wa Marudio’ kufuatia tamko binafsi la Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC), Jecha Salim Jecha, alilolitoa tarehe 28/10/2015 kwamba ameufuta Uchaguzi Mkuu wa tarehe 25/10/2015 na matokeo yake yote.
Tangazo hilo la Jecha Salim Jecha, lililo kinyume na Sheria ya Uchaguzi ya Zanzibar Nam. 11 ya 1984 na linalopingana na Katiba ya Zanzibar, lilikuja baada ya waangalizi wote wa Uchaguzi wa ndani na wa kimataifa ikiwa ni pamoja na Umoja wa Ulaya (EU), Jumuiya ya Madola (The Common Wealth), Umoja wa Afrika (AU), Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC), Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), na Waangalizi wa Marekani na Uingereza, kutoa taarifa zao na kueleza kuridhishwa na mwenendo wa Uchaguzi huo na kwamba ulikuwa huru na wa haki kwa sababu ulifuata taratibu za kisheria na ulifanyika kwa amani.
Aidha, baada ya kukamilika kwa hatua ya upigaji kura, wadau na washiriki wa ndani wa uchaguzi huo akiwemo, yeye mwenyewe, Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar, mgombea Urais wa Chama Cha Mapinduzi CCM, Dk. Ali Mohamed Shein, mgombea wa Urais wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad na wagombea kutoka vyama vyengine walikiri kwamba uchaguzi ulikuwa huru na wa haki.
Ghafla, kutokana na shindikizo kubwa kutoka kwa viongozi wa Chama chake, ambacho aliwahi kuomba ridhaa ya kugombea Ubunge kupitia chama hicho na kuanguka katika hatua ya kura za maoni, Mwenyekiti wa Tume alitangaza kuufuta Uchaguzi huo kwa kutumia hoja na maelezo yaliyotolewa na CCM baada ya kubaini imeshindwa kwenye nafasi ya Urais wa Zanzibar.
Tokea kutolewa kwa tangazo hilo kumekuwepo na juhudi mbalimbali ndani na nje ya nchi za kutafuta suluhisho kutokana na mgogoro ulioibuliwa kwa makusudi kwa lengo la kukinusuru Chama Cha Mapinduzi CCM kuondokana na aibu ya kushindwa katika Uchaguzi Mkuu wa 25 Oktoba 2015.
Miongoni mwa juhudi za ndani ni pamoja na Mgombea Urais wa Zanzibar kupitia CUF, Maalim Seif Sharif Hamad, kukutana na viongozi mbalimbali akiwemo mgombea Urais wa Zanzibar kupitia CCM, Dr. Ali Mohamed Shein, Marais wastaafu wa Zanzibar, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, John Pombe Magufuli na Mwenyekiti wa CCM, Jakaya Kikwete ili kufanya mazungumzo na kuiepusha nchi kutokana na migogoro na mifarakano ya baada ya uchaguzi. Viongozi wa dini mbalimbali nao pia walichukua dhamana na dhima ya kuhakikisha kuwa mgogoro wa Zanzibar unapatiwa ufumbuzi kwa lengo la kuibakisha Zanzibar katika hali ya umoja na masikilizano miongoni mwa wananchi wake.
Kwa upande wa juhudi za nje, jumuiya ya kimataifa imesikika mara kadhaa ikitoa matamko na kuchukua hatua mbalimbali kuitaka Tume ya Uchaguzi kukamilisha kazi ya uhakiki na majumuisho ya matokeo ya uchaguzi na kumtangaza mshindi. Jumuiya hiyo pia iliushauri uongozi wa vyama vya CCM na CUF kukaa pamoja kuzungumza jinsi ya uundwaji na uendeshaji wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar kama yalivyo matakwa ya Katiba ya Zanzibar na kuhakikisha kuwa demokrasia, haki za binadamu na amani vinaenziwa, kulindwa na kutunzwa. Kwa makusudi na kwa lengo maalum, hatua zote hizo zimepuuzwa na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar na Serikali zote mbili, na hatimaye Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar alitangaza kufanyika kwa kile kinachoitwa Uchaguzi wa Marudio uliopangwa kufanyika tarehe 20 Machi 2016.
Kupuuzwa huko kwa juhudi za ndani na nje, kunakochochewa na baadhi ya viongozi waandamizi wa CCM na Serikali zote mbili, Baraza Kuu la Uongozi la Taifa la The Civic United Front (CUF-Chama Cha Wananchi) lililokutana katika kikao cha dharura tarehe 07 Novemba, 2015, mjini Zanzibar kuzungumzia hali ya kisiasa hapa nchini kufuatia Uchaguzi Mkuu wa tarehe 25 Oktoba, 2015 lilifikia maamuzi ya kuitaka Tume ya Uchaguzi, pamoja na mambo mengine, irudi kukamilisha hatua zilizobaki za uhakiki na majumuisho ya matokeo ya Uchaguzi. Kimsingi, Baraza Kuu lilisisitiza halitakubaliana, kwa namna yoyote ile, na hatua ya kufanya Uchaguzi wa marudio kwa kuzingatia kukosekana kwa uhalali wa kisheria katika ufutwaji wa matokeo ya Uchaguzi na kwamba uchaguzi ulishafanyika na kazi ya kuhesabu kura kumalizika.
Tokea kutolewa kwa tamko la kufutwa kwa Uchaguzi, kutangazwa kwa Uchaguzi wa marudio, na kutolewa kwa Azimio la Baraza Kuu la Uongozi la CUF, Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imejikuta katika taharuki na wasiwasi mkubwa na kupelekea khofu isiyomithilika kuhusiana na hali ya kisiasa na kiusalama ya Zanzibar. Kwa mfano, kumeripotiwa matukio mengi ya uvunjwaji wa haki za binadamu ambapo raia wasio na hatia wanapigwa na kujeruhiwa vibaya, nyumba na makaazi ya watu kuvunjwa na kuchomwa moto, maeneo ya vyama vya siasa, kama vile barza za CUF, yamehujumiwa kwa kuchomwa moto na ofisi zake kuvunjwa na kuibiwa mali zote kabla ya kuwashwa moto na kuteketea kabisa. Kwa mfano, siku ya Jumatatu, tarehe 15, Machi 2016, makundi ya askari wakiwa na silaha za moto walivamia ofisi ya Chama Cha Wananchi CUF iliyopo katika eneo la Mpendae na kuvunja na kuiba vifaa mbalimbali vya ofisi hiyo zikiwemo kompyuta, printers na photocopy machines.
Katika tukio hilo, maharamia hao walivunja eneo linalotumika kuhifadhia vifaa vya muziki na kuiba vifaa vyote vya BRASS BAND ya CUF. Mengi ya matukio haya yamefanywa na kikundi kidogo cha askari wa vikosi vya SMZ, ambacho hutumia magari yenye namba za usajili za SMZ na silaha za moto na kujifunika nyuso zao kwa staili ya ninja kilichoandaliwa maalum kwa ajili ya kuwahujumu raia, wakisaidiwa na vyombo vya Ulinzi na Usalama vya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Sambamba na hujuma hizi kumeibuka mtindo wa kuwatisha raia kwa kuwavamia kuwapiga na kuwabambikizia kesi kwa lengo la kuwashikilia katika vituo vya Polisi, kinyume na utaratibu wa kisheria, na kuwadhalilisha kwa kuwapiga na kuwatolea maneno ya vitisho na matusi. Katika uvamizi uliofanywa katika ofisi ya CUF ya Mpendae, zaidi ya vijana 30 walikamatwa na jeshi la Polisi, lililoshiriki katika uhalifu huo kwa lengo la kuwapatia ulinzi maharamia waliopewa kazi ya kuhujumu ofisi hiyo, na kuwarundika katika vituo vya Polisi na kuwanyima dhamana.
Mkakati wa kuwatisha raia ulielekezwa pia kwa viongozi wa CUF. Tarehe 16 Machi 2016, Jeshi la Polisi lilivamia nyumbani kwake na kumkamata Kaimu Mkurugenzi wa Habari, Uenezi na Mawasiliano kwa Umma, Mheshimiwa Hamad Masoud na kumuweka ndani na kumnyima dhamana. Tukio hili la kukamatwa Mheshimiwa Hamad Masoud linafuatia kuwekwa ndani na kunyimwa dhamana kwa aliyekuwa mjumbe wa Timu ya Kampeni inayojulikana kama Timu ya Ushindi ya Chama Cha Wananchi (CUF) ndugu Mohamed Ahmed Sultan Al-Mugheir (Eddy Riyami) tarehe 16, Februari 2016 na kuitwa Polisi Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Mheshimiwa Nassor Ahmed Mazrui tarehe 3 Machi, 2016 kwa kuwataka wanachi wajilinde kutokana na kushamiri kwa vitendo vya hujuma dhidi ya wafuasi wa vyama vya upinzani vinavyofanywa na makundi tuliyoyataja. Vilevile, jana tarehe 17 Machi, 2016 aliyekuwa Mjumbe katika Timu ya Ushindi ya CUF na Mgombea Uwakilishi wa jimbo la Chukwani, Mheshimiwa Mansour Yussuf Himid, aliitwa na Jeshi la Polisi kwa madhumuni ya kuhojiwa.
Sambamba na haya, kumekuwepo na juhudi kubwa zinazoongozwa na Mamlaka mbalimbali ikiwemo Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kuvishurutisha vyama vya siasa, hasa vile vilivyotangaza waziwazi kugomea Uchaguzi wa marudio, kushiriki katika uchaguzi huo kwa lengo la kuhalalisha mkakati ulioandaliwa wa kulazimisha ushindi wa CCM ambao waliukosa katika uchaguzi wa tarehe 25 Oktoba, 2015.
Kwa mfano, tarehe 25 Januari, 2016, Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar iliwasilisha Makao Makuu ya CUF barua yenye kumbukumbu TUZ/78/16/2015/2016/Vol.I/2 kwa lengo la kutoa taarifa kuhusu uchaguzi wa marudio. Kutokana na barua hii, CUF, kupitia Naibu Katibu Mkuu, Mheshimiwa Nassor Ahmed Mazrui, iliiandikia Tume barua yenye kumbukumbu namba CUF/HQ/AKM/ZEC/037/016/055 ya tarehe 05/02/2016 kujibu barua ya Tume ya tarehe 4 August, 2015 yenye kumbukumbu TUZ/78/2015/2016/VOL.VI/68 na barua ya kukumbushia barua yake ya tarehe 17, August, 2015 yenye kumbukumbu CUF/HQ/AKM/ZEC/037/015/032.
Kwa barua yake ya tarehe 5 Februari, 2016 CUF iliitaarifu Tume ya Uchaguzi juu ya maazimio ya Baraza Kuu la Uongozi la Taifa kutoshiriki katika Uchaguzi ambao umetangazwa kufanyika tarehe 20/03/2016 kwa sababu kufutwa kwa uchaguzi wa tarehe 25 Oktoba, 2015 ni batili na kwa hivyo marudio ya uchaguzi wa tarehe 20 Machi 2016 ni batili pia, na ni kinyume na Katiba ya Zanzibar na Sheria ya Uchaguzi ya 1984.
Aidha, kwa barua hiyo, CUF iliitaka Tume ya Uchaguzi Zanzibar, kutokana na Azimio la Baraza Kuu la Uongozi, kuondoa majina ya wagombea wake wote, akiwemo Maalim Seif Sharif Hamad, katika orodha ya wagombea wa Uchaguzi huo na vile vile yasiingizwe katika karatasi za kura kwa uchaguzi wa marudio.
Zaidi, tarehe 8 Februari, 2016 Naibu Katibu Mkuu wa CUF aliwasilisha barua, kwa Tume ya Uchaguzi Zanzibar, iliyokuwa na lengo la kuelezea msimamo wa CUF kuhusiana na kufutwa isivyo halali kwa uchaguzi wa tarehe 25 Oktoba 2015 na kuitishwa kwa kile kinachoitwa uchaguzi wa marudio wa tarehe 20 Machi, 2016.
Kwa barua hiyo pia, CUF ilibainisha mapungufu ya kisheria na ukiukwaji wa Katiba ya Zanzibar katika tangazo la kufutwa kwa uchaguzi na kwa hivyo kutothibitisha mgombea yoyote katika ngazi zote za uchaguzi wa zanzibar kama ilivyotakiwa kufanya na Tume ya Uchaguzi. CUF iliikumbusha Tume na kusisitiza juu ya uamuzi wake wa kuitaka tume kuhakikisha haitumii jina, alama, wala picha ya mgombea yoyote kupitia CUF katika karatasi za kura.
Hata baada ya rundo la barua hizi za CUF, zenye lugha rahisi na maelezo yanayojitosheleza, kwa Tume ya Uchaguzi kukataa kushiriki katika batili iliyopachikwa jina la uchaguzi wa marudio, tarehe 29 Februari 2016, Tume ya Uchaguzi, kwa mara nyingine tena, iliiandikia CUF barua yenye kumbukumbu namba TUZ/78/16/015/016/VOL. I/200 kuitaka CUF kuwasilisha majina ya mawakala wake katika uchaguzi ambao kimsingi walishautolea msimamo.
CUF kwa upande wake ilimwandikia Mkurugenzi wa uchaguzi barua yenye kumbukumbu CUF/HQ/AKM/ZEC/037/016/056 ya tarehe 03 Machi 2016 kukumbushia msimamo wake wa kutoshiriki Uchaguzi huo na kwamba kutokana na uchaguzi huo kukosa uhalali kisheria na kikatiba, haioni haja ya kuwasilisha majina ya waangalizi kwa uchaguzi huo. Kwa mara nyingine tena, tarehe 8 Machi 2016, Tume iliiandikia CUF barua yenye kumbukumbu TUZ/78/16/2015/2016/VOL.II/6 kutoa taarifa kuhusu kuwasili kwa karatasi za kupigia kura kwa ajili ya Uchaguzi wa marudio wa tarehe 20 Machi 2016 na kuitaka CUF kutuma majina mawili ya watakaoshiriki katika mapokezi ya karatasi hizo. Bila ya shaka, Tume imo katika mpango wa kuilazimisha na kuishurutisha CUF, hata kama haitaki, kushiriki katika uchaguzi huo kama inavyothibika katika hatua mbalimbali za Tume hiyo ikiwa ni pamoja na kuchapicha majina, nembo na picha za wagombea wa CUF katika karatasi za kura kwa ajili ya uchaguzi wa marudio hata baada ya CUF kukataa kushiriki katika uchaguzi huo
Tukiwa tunakaribia siku ya Uchaguzi wa marudio, CUF imebaini njama kadhaa mpya zinazoratibiwa na baadhi ya viongozi wa CCM na kutekelezwa na baadhi ya watendaji wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar. Miongoni mwa mbinu hizo ni pamoja na kutoa vitisho kwa wafanyakazi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na askari wa vikosi vya Idara Maalum ya Zanzibar na askari wa majeshi yaliyo chini ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Polisi na Jeshi la wananchi wa Tanzania (JWTZ) waliopo Zanzibar, ya kuhakikisha wanajitokeza kwa lazima katika uchaguzi wa marudio na kuipigia kura CCM.
Pia, kumekuwepo na mpango wa kuandaliwa kwa mawakala ‘feki’. Katika hili Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar inashirikiana kwa karibu na kwa kiasi kikubwa na baadhi ya watendaji wa serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, wakiwemo viongozi wa vikosi vya idara maalum, kuandaa watu, ambao wengi wao ni askari wa vikosi hivyo, watakaopewa vitambulisho vinavyowaonesha kuwa ni mawakala wa CUF, na kutumia majina ya mawakala wa CUF wa 25 Oktoba 2015, na kusambazwa katika maeneo yote ya Uchaguzi nchi nzima. Lengo la mpango huu ni kutaka kuwahadaa wanachi kuwa CUF ilishiriki Uchaguzi kwa kuwa ilitoa mawakala walioshiriki katika Uchaguzi. Pia, mpango huu unalenga katika kuzusha hali ya kutofautiana miongoni mwa uongozi wa CUF na wanachama wa kawaida ili ionekane uongozi wa juu wa CUF umewasaliti wananchi katika dakika za mwisho kuelekea uchaguzi wa marudio.
Kwa upande mwengine, CCM yenyewe imekuwa inaongoza mkakati maalum wa kuwatafuta baadhi ya waliokuwa mawakala wa CUF katika uchaguzi wa terehe 25 Oktoba 2015, na kuwapa fedha nyingi ili wakubali kuwa mawakala wa CUF katika uchaguzi wa marudio wa tarehe 20 Machi 2016. Ili kuhakikisha lengo la kuwatumia mawakala hao kufanikisha mchezo wao mchafu waliouanza mara tu baada ya kufutwa kwa uchaguzi wa tarehe 25 Oktoba, 2015, CCM imekuwa ikiwazaini mawakala hao wa CUF kwa ahadi mbalimbali za fedha na vitu vya thamani.
Kutokana na hayo yote tuliyoyaeleza kwa kina, CUF-Chama Cha Wananchi:
• Kinatoa wito kwa wananchi wote kufuata kwa umakini na ukamilifu maelekezo na kauli za viongozi wazalendo, wanaoitakia mema nchi hii kwa kuchukua juhudi kubwa kuinusuru na mifarakano ya aina zote, kususia kile kinachoitwa uchaguzi wa marudio unaotarajiwa kufanyika siku ya Jumapili, tarehe 20 Machi, 2016 kwa kukaa majumbani mwao kwa utulivu na kujiepusha na mikusanyiko isiyo ya lazima ili kujikinga na dhamira na matendo maovu ya kiharamia yaliyopangwa na kikundi cha wahuni wachache wa kisiasa dhidi ya raia wasio na hatia.
• Kinawafahamisha na kuwatanabahisha wafuasi wake na wananchi wengine wote walioamua kuchagua mabadiliko ya kiuongozi katika nchi yetu katika uchaguzi uliopita kwamba haijawasilisha jina hata moja la mtu yoyote kama mapendekezo yake kwa ajili ya mawakla watakaotumika katika uchaguzi wa marudio wa tarehe 20 Machi, 2016 kwa hivyo haitokuwa na wakala hata mmoja kwa ngazi yoyote katika uchaguzi wa tarehe 20 Machi, 2016. Ni muhimu kwa wanachi kuachana na propaganda zilizopitwa na wakati zinazoenezwa na CCM kuhusu mikakati ya CUF kuelekea 20 Machi, 2016.
• Mbali na kutoshiriki uchaguzi wa marudio unaosimamiwa na ZEC, pia CUF inawataka wanachama, wafuasi wake na wananchi wote kutoshiriki katika uchaguzi wa marudio katika Jimbo la Kijitoupele unaosimamiwa na Tume ya Tiafa ya Uchaguzi (NEC). CUF inawataka wananchi kususia uchaguzi huo kwa sababu kwa Zanzibar ni ZEC ndio hufanya kazi kama wakala wa NEC, hivyo hakuna haki itakayotendeka katika uchaguzi huo.
• Kinawataka wananchi wote kufahamu kuwa suala la kushiriki uchaguzi ni suala la mtu binafsi na hakuna mtu au mamlaka yoyote yenye uwezo wa kulazimisha watu kushiriki katika suala hilo. Chama kinawataka wananchi kuwa watulivu na kuondoa khofu kutokana na idadi kubwa ya askari wa JWTZ na Polisi wanaoranda randa mitaani wakiwa na silaha nzito. CUF inawaomba wananchi kubaki na msimamo wao wa kutoshiriki uchaguzi.
• Kinawasihi wale wote waliotishwa kwa kunyang’anywa vitambulisho vyao vya Mzanzibari na vitambulisho vya kupigia kura, kutotishika na hatua zinazochukuliwa sasa na watendaji waandamizi wa SMZ na mawakala wao kwa kukataa dhulma na kutumiliwa nguvu katika mambo yaliyo chini ya khiari zao. Pia, CUF inawasihi wananchi hao kuonesha msimamo wao katika kulinda na kutetea haki zao za kikatiba na kuonesha mapenzi yao kwa nchi yao kwa kukataa ukiukwaji wa Katiba na uvunjwaji wa Sheria za nchi yetu kwa kushiriki katika ukandamizaji na uvizwaji wa demokrasia nchini.
• Kinawakumbusha askari wa vikosi vyote, walio na uchungu na mapenzi mema na nchi yetu, kukataa kutumiwa na wanasiasa walioweka mbele maslahi yao binafsi na kuusahau umma wa wananchi wanyonge wa nchi hii. Ni vyema kwa askari hawa kutambua kuwa wao ni sehemu ya jamii yetu na kwamba shida na maisha magumu tuliyonayo yanawahusu na kuwakumba kama raia wengine wote. Kukataa kwao kuwa ngazi ya viongozi wanaotafuta hadhi na heshima kwa kupitia migongo ya wengine kutawatoa wao katika idhilali ya kutumika kila nyakati za uchaguzi zinapowadia na kutelekezwa hadi kipindi kama hicho baada ya miaka mitano ambapo hutafutwa na kupewa tena ahadi kemkem zisizotekelezwa.
• Kinamnasihi Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa John Pombe Magufuli kutambua kuwa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), lililo chini ya amri yake kama Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama, linaendesha vitisho kwa wananchi kutokana na kuonekana kwa wingi wakiwa na silaha nzito katika maeneo ya wananchi. CUF inamtaka Mheshimiwa Magufuli kuondosha majeshi yake yanayoshirikiana na Polisi na vikosi vya SMZ kuendesha unyanyasaji na udhalilishaji wa raia wasio na hatia.
CUF-Chama cha Wananchi kinawataka wanachama, wafuasi wake na wananchi wote waliochagua mabadiliko ya uongozi wa kisiasa katika nchi yetu na kuonesha msimamo wao wa kuikataa CCM kupitia sanduku la kura tarehe 25 Oktoba, 2015 kutovunjika moyo na siasa uchwara zinazoendeshwa na CCM kwa lengo la kuwatoa katika mstari wa kupigania ushindi wetu mkubwa tulioupata. Tunawahakikishia kuwa subra zao na jitihada kubwa inayochukuliwa na Viongozi wa Chama Chetu vitachochea kufikiwa kwa malengo.