Tuesday 30 June 2020

KAMA HATUKUSEMA NANI ATASEMA BLOGGER  AMEAMUA KUAYANIKA LEO

RAIS MAGUFULI NAKUOMBA SOMA HAYA ILI USIINGIZWE MKENGE. JINSI TEAM YA MAWAZIRI WA ZANZIBAR WALIVYODHAMIRIA KUMUANGUSHA WAZIRI WAKO  MCHAPAKAZI MAKAME MBARAWA ASIWE MGOMBEA WA CM ZANZIBAR

Zanzibar mwaka huu wanategemea kupata Rais mpya wa awamu ya 8 tangia mwaka 1964 baada ya Mapinduzi matukufu ya Zanzibar.

Zanzibar wamepita Marais wengi sana na kwakweli kila mmoja wao yapo mengi mazuri kwa kila mmoja kwa nafasi yake aliyafanya akiwa kama kiongozi Mkuu wa Zanzibar.

Lakini katika Uchaguzi wa mwaka huu, kumejitokeza mambo mengi sana katika harakati za Wanachama wanaotaka kuchaguliwa na Chama na baadae Wananchi wa Zanzibar ili kuiongoza Zanzibar katika kipindi cha miaka 5 kwa maana 2020/2025.

Dhana ya kibaguzi imeanza kuchipua ndani ya Chama Cha Mapinduzi hasa Zanzibar baada takriban miaka 15 visiwani hapa kuwa eneo tulivu na kupungua kwa chuki ambayo ilishamiri sana miaka ya 1985 mpaka 1995 kipindi ambacho siasa za Uunguja na Upemba zilishamiri sana visiwani hapa.

Lakini baada ya kuingia Amani Karume na baadae Dr. Shein hali ya ubaguzi ya Uunguja na Upemba ilipungua sana na hapa lazima tuwapongeze Viongozi wawili hawa.

Lakini Uchaguzi wa mwaka huu kumeanza kuibuka masuala ya kibaguzi ndani ya CCM hasa suala la wana CCM wanaofanya kazi kwenye Serikali ya SMT na wale wa SMZ kwa maana Viongozi wanaofanya kazi kwenye   Serikali ya Dr. John Pombe Magufuli na Dr. Ali Mohamed Shein.

Na hapa tutakuwa wazi kabisa kuelezea kiini cha ubaguzi huu ni nini?

Kwa miaka mingi sana Zanzibar imeliwa sana, watu wamejilimbikizia mali, ardhi na wengine wamejilimbikizia mali za Serikali hasa hawa Viongozi wanaofanya kazi kwenye Serikali ya SMZ na wale ambao walishawahi kufanya kazi Zanzibar.
Hofu yao kubwa ni kuogopa yanayotokea Bara yasije kuhamia huku kwa maana Viongozi mbalimbali kuanza kuhojiwa na vyombo vya sheria juu mali zake na vitu vya namna hiyo. Kwahiyo kwa hofu hiyo kumetengenezwa mtandao ukiratibiwa na mmoja ya Waziri anayefanya kazi karibu na Rais na mwingine anayefanya kazi karibu na Makamo wa pili wa Rais kuhakikisha wanaunajisi uchaguzi wa ndani ya Chama kwa kuhakikisha yeyote anayetoka kwenye Serikali ya SMT basi asiwe na asifanikiwe kushinda ndani ya Chama na wameenda mbali zaidi kumuhusisha na Rais Shein kuwa yupo nao kwenye mpango wao huo wakati kiuhalisia Rais Shein hayuko nao na hajatoa baraka zozote za hayo wanayoyafanya.

Viongozi hao kwanza walianza kusema viongozi wanaotoka SMT hawatakiwi na Wananchi wa Zanzibar na kuwasingizia Wananchi wa Zanzibar kwamba hawawataki baadhi ya Viongozi wanaofanya kazi kwenye Serikali ya Rais Magufuli lakini baada ya kujichimbia Zanzibar miezi miwili nikifanya tafiti juu ya nani anayefaa kuwa Rais wa Zanzibar nikagundua mambo mengi sana na mengine ya hovyo kabisa kwa maslahi ya CCM na Zanzibar.

Hawa Viongozi wamekuwa wakitumia sana jina la Rais Shein kwamba ana mtu na wakimtaja Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha kama ndiye chaguo lake. Mchezo huo unafanywa na Waziri wa karibu na Rais.
Na huyu bwana amekuwa akiendesha mikakati mingi sana na kikundi chake kuhakikisha idadi ya watu wengi sana wanaenda kuchukua fomu za kuomba ridhaa ili idadi ya wanaofanya kazi SMZ iwe kubwa zaidi ya wale wanaofanya kazi SMT nia yao ni kukipa ugumu Chama kwenye kuteuwa nani awe.

Hawahawa walipoona Profesa Mbarawa ametoka Pemba na amekuwa Mpemba pekee kuchukua form wakaona atakuwa na nafasi kubwa ya kuingia tatu bora, wanaume hawa hawajipanga ili kumuondoa kwenye matumaini hayo Profesa, wakakubaliana Mhe. Mjawire na Mohammed Abood wakachukue form ili asiwe peke yake kutoka Pemba na kuweka ugumu wa kupenya na kwakweli wamefanikiwa kwenye hilo, maana pamoja na Changamoto za Ndoa yake Profesa kwamba mkewe si Mtanzania lakini alikuwa na nafasi ya kuingia kwenye tatu bora. Hawa ni mafia wa Zanzibar lazima watizamwe sana.

Lakini hiki kikundi kimeshawishi watu wengi sana kuchukua form na wengi walishangaa kumuona aliyewahi kuwa Waziri wa Fedha Zanzibar Mhe. Dr Khalid Salum kuchukua form na siku ya pili Katibu Mkuu wake naye akaenda kuchukua form. Haya yote ni mipango iliyosukwa na kikundi kisichotaka mabadiliko Zanzibar, kisichotaka Mapinduzi ya uongozi na kifikra Zanzibar kikundi ambacho kinataka kiendelee kuwepo kwenye Serikali. Hawa wamekuwa wakiwasingizia Wananchi wa Zanzibar kwamba hawawataki Viongozi fulani na wakisema hawana mvuto lakini kiukweli hilo halipo sema ni propaganda iliyotengenezwa ili kukipa hofu Chama kisiteuwe Viongozi wanaotoka SMT ili wao waendelee kuneemeka.

Kikubwa kinachowasumbua hawa ni hofu, hofu ya vyeo na mali walizochuma. Wanaogopa kiongozi akitokea SMT ataleta mambo ya Magufuli Zanzibar na wao wameshazoea kula na vyeo vya kupeana na wamekuwa wakisema na kusingizia Wananchi kwamba kiongozi akitokea SMT Wananchi watasusa kupiga kura huu ni uongo na uzandiki mkubwa sana.

Hawa wamekuwa wakifanya kila hujuma ili mambo yao yaendelee kulindwa.
Na kama kuna kosa kubwa litafanywa na Wazanzibar (CCM ) ni kuteuwa hawa Viongozi wetu tunao waona kila siku. Kama Zanzibar tunataka mabadiliko basi lazima aje mtu atakayetuondoa hapa tulipo, mtu ambaye hataona haya na kufumbia macho  mambo ya hovyo na kikubwa awe na hekima na busara za kuweza kufanya kazi kwa karibu na Rais Magufuli.

Zanzibar ina nafasi kubwa sana ya kutoka hapa ilipo ikiwa atakuja kiongozi mwenye maono na aliyetosheka.

Hawa Viongozi wetu wa hapa hawana jipya la kuwafanyia Wazanzibari zaidi ya kuendeleza yaleyale ya siku zote. Zanzibar inataka mtu mpya mwenye maono na utulivu wa Kiuongozi.

Lakini kikubwa sana CCM na hasa Rais Magufuli awaangalie sana hawa Wanachama walichukua form kwa umakini wa hali ya juu sana.
Mtaona kundi kubwa sana la watu lakini ile ilikuwa tashtiti wanamtisha Mwenyekiti wa Chama kwamba wao wana watu wa kutosha wenye sifa za kuwa Marais Zanzibar, lakini hawa pamoja na wingi ule lakini ni wamoja na wamekubaliana yeyote atakayepita katika wale wa SMZ watakuwa naye ili kuendelea kulinda maslahi yao.

Hili ni zoezi limeratibiwa ili kuendeleza mtandao wao, wamechukua form wengi lakini ni wa moja ni watu wamoja wamekubaliana.
Na hawana ajenda nzuri kwa Zanzibar na CCM.

Lakini wengi wao katika hawa hawaridhishwi na Mwenyekiti wa CCM kwasababu hawataki kuingiliwa, wanahisi Rais Magufuli atakuwa anatoa maelekezo kule na wao hawataki.
Wanataka waendeleze ulaji wao na mambo yao ya kila siku.

Na leo nasema jambo hapa na iko siku mtakuja kulithibitisha. CCM lazima wamtafute mtu atakayeweza kufanya kazi na Rais Magufuli kwa uaminifu mkubwa sana.
CCM wakikosea hapa kwenye mchakato huu kutatokea mgogoro mkubwa wa Muungano hasa hawa wahafidhina wa Zanzibar wakifanikiwa kushika Nchi hawatosikia lolote kutoka Bara. Na nia yao ni ovu sana wanataka kumuonyesha Rais Magufuli kwamba wao hawaendeshwi na Zanzibar ni Nchi.
Hili CCM waache ubinafsi lazima wamjue Mwenyekiti wao ni mtu wa namna gani na anapaswa awe na pacha kwa Zanzibar wa namna gani. Wakikosea kwenye hili tutakuwa tumeweka rehani Muungano. Ni muhimu CCM wajue Mwenyekiti wao hapendi wababaishaji na hawa wa huku kwetu ni wababaishaji watamvuruga tu.

Lazima kazi ifanyike na hasa CCM Bara isiwaachie CCM Zanzibar jukumu la Kusimamia Uchaguzi ni hatari mno kwa masilahi ya Nchi na CCM.
Hawa viongozi wa CCM Zanzibar baadhi wamesha ahidiwa vyeo kwahiyo ikitokea ametoka mgombea kutoka SMT wengi wao watanuna na huu mchezo lazima ukomeshwe.
Kitengenezwe kikosi kazi kizuri kipya kikashirikiane na wale wa Kisiwandui wasimamie ushindi wa CCM na siyo kuwaachia wale pekee wa Kisiwandui.
Vinginevyo yatatokea mambo ya ajabu sana na hamtokuja kuamini.
Watu wamejawa na tamaa, chuki na kulipiza kisasi hasa kuna baadhi wanaamini walinyanyaswa na Rais Magufuli na kusabisha watolewe kazini, na wengine wana amini Dr. Shein amekuwa mtu soft sana kwa Rais Magufuli.
Kwahiyo wao wamejipanga si kwa maslahi ya Zanzibar bali kulinda masilahi yao na ndiyo maana wamehakikisha wanakuwa na idadi kubwa ili kutuma ujumbe kwa Mwenyekiti wa Chama.

CCM NA RAIS MAGUFULI ANGALIE MSIINGIE  KWENYE MTEGO HUU.

Mwandishi
KOMBO HAMDUNI KOMBO

No comments: