Sunday 1 March 2015

Mkoa Wa Lindi October 2015 Jino kwa Jino

Leo tunaianza rasmi safari ya Mkoa wa Lindi baada ya kumaliza uchambuzi wa majimbo 41 yaliyo katika mikoa ya Dar es Salaam, Dodoma, Mara, Kigoma na Kilimanjaro.
UJUE MKOA WA LINDI
Mkoa wa Lindi uko kusini mwa Tanzania na umepakana na mikoa ya Pwani, Mtwara, Ruvuma, Morogoro. Upande wa mashariki hupakana na Bahari Hindi” Bahari ya Hindi. Mkoa huu ulianzishwa mwaka 1971 na una eneo la kilometa za mraba 67,000.
Karibu robo ya eneo la Mkoa wa Lindi (Kilometa za mraba 18,000) ni sehemu ya Hifadhi ya Wanyama ya Selous, moja ya vivutio vikubwa vya utalii lakini hifadhi hii haijatangazwa ipasavyo ili kulisaidia taifa mapato ya kutosha. Kivutio kingine kilichoko Lindi ni mito mikubwa ya Lukuledi, Matando na Mavuji ambayo yote inaeleka Bahari Hindi bila kusahau miji ya kale ukiwemo ule wa Kilwa Kisiwani ambao ni wa kihistoria kwa pwani ya Afrika ya Mashariki. Pia kuna magofu muhimu ya kale yanayoonesha namna gani mji huo wa Kilwa ulivyowahi kuwa kitovu cha biashara karne nyingi zilizopita.
Mkoa una wilaya sita za Lindi Mjini, Lindi Vijijini, Kilwa, Nachingwea, Liwale na Ruangwa pamoja ya majimbo manane ambayo ni Lindi Mjini, Ruangwa, Kilwa Kaskazini, Kilwa Kusini, Liwale, Nachingwea, Mchinga na Mtama.
Wakazi
Kwa mujibu wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012, Mkoa wa Lindi una jumla ya wakazi 864,652 huku asilimia 90 kati yao wakiwa ni wakulima. Makabila makubwa yaliyojikita ni Wamwera ambao hasa hupatikana wilaya za nachingwea na katika baadhi ya tarafa za Lindi Vijijini. Pia kuna Wamachinga na Wamalaba ambao wako zaidi Lindi Mjini bila kusahau Wamatumbi na Wangindo ambao wanapatikana Kilwa.
Miundombinu ya Mawasiliano
Kwa sababu Lindi ni mkoa ulioko kusini mwa Tanzania, maendeleo yamekuwa kwa mwendo wa jongoo kutokana na kukosekana kwa barabara ya uhakika kwa miongo mitano tokea nchi yetu ipate uhuru. Ni hivi sasa tu ndipo mawasiliano kati ya wana Lindi na Mikoa mingine ya Tanzania yameimarika, hasa baada ya kukamilika kwa ujenzi wa daraja la Mkapa mwaka 2002.
Ukosefu wa barabara za uhakika uliodumu kwa miaka mingi umeathiri uchumi wa Lindi ikiwemo Miradi mbalimbali ya maendeleo ambayo ilishakufa “kifo cha mende”.
Lindi kuna bandari ambayo imetelekezwa bila kuendelezwa huku Gesi iliyopatikana baharini karibu na Kisiwa cha Songosongo ikiwa haina manufaa makubwa kwa wana Lindi na Taifa kwa ujumla. Ukimuuliza raia yeyote wa Lindi gesi ile imemnufaishaje hakuna anayejua, mikataba yake iliingiwa kwa siri na ni vigumu kwa mtu mwingine kujua nini kinaendelea huko.
endelea http://www.mwananchi.co.tz/kolamu/-/1607214/2638458/-/item/1/-/10hsdgkz/-/index.html

No comments: