Tuesday 25 August 2015

POLISI WASIPOKUWA "MAKINI" WATAHARIBU AMANI YA NCHI.

Waziri wa zamani wa mambo ya Ndani Mhe.Lawrance Masha leo amepandishwa ktk mahakama ya hakimu mkazi Kisutu akituhumiwa kutoa lugha ya kuudhi (Abusive Language) dhidi y Mkaguzi msaidizi wa Polisi Juma Mashaka wa kituo cha Polisi cha Oysterbay jijini Dar.

Masha anatuhumiwa kutoa maneno hayo ya kuudhi ambayo ni kinyume na kifungu cha 89 (i) (a) cha kanuni za adhabu (Penal Code [cap 16 R.E 2002].

Maneno anayodaiwa kutumia ni; "nyie polisi ni wapumbavu, waonevu hamna shukrani wala hamna dini"

Maneno haya yanasemekana kumuudhi Mlalamikiwa hali iliyosababisha Masha kukamatwa, kufunguliwa mashtaka na leo kupandishwa kizimbani ktk mahakama ya hakimu mkazi Kisutu ili kujibu tuhuma hizo.

Kesi hiyo imepewa shtaka namba 190 la mwaka 2015. Mlalamikaji ni Jamhuri, aina ya kosa ni lugha ya kuudhi (Abusive Language) ambapo kwa mujibu wa hati ya mashtaka ni kosa la jinai (criminal offence).

ILIVYOKUWA;

Jana majira ya jioni Polisi mkoa wa Dar waliwakamata vijana 19 kwa madai kuwa wamefanya mkusanyiko usio halali na wanapanga kuandamana.

Wanafunzi hao walipelekwa kituo cha Polisi Oysterbay na kuwekwa rumande wakisubiri kupandishwa mahakamani kujibu tuhuma za kufanya mkusanyiko usio halali (unlawful assembly) na kula njama ya kutaka kuandamana.

Waziri Masha alipewa taarifa hizo na akafika kituo cha Polisi Oysterbay ili kuwawekea dhamana vijana hao ambao wanadaiwa ni wanafunzi lakini, Jeshi la Polisi limekataa kutaja ni wanafunzi wa wapi.

Alipofika kituoni hapo Masha anadaiwa kutoa lugha ya kuudhi kwa Askari Polisi hali iliyomfanya akamatwe na kuwekwa rumande pamoja na wanafunzi alioenda kuwawekea dhamana.

Leo wamepandishwa kizimbani ktk Mahakama ya hakimu mkazi Kisutu ambapo Masha ameshtakiwa kwa kutumia lugha ya kuudhi dhidi ya Polisi na wanafunzi hao wameshtakiwa kwa kufanya mkusanyiko usio halali (Unlawful Assembly).

Watuhumiwa wote wamerudishwa Rumande baada ya kushindwa kutimiza masharti ya dhamana. Hata hivyo watuhumiwa hao wanatetewa na Mwanasheria mashuhuri Nchini na Afrika Mashariki Peter Kibatala.

MASWALI MUHIMU.!

1. Hivi kusanyiko la watu 19 linaweza kuhesabika kama ni "Unlawful assembly"? Kama ndivyo basi watu wasiende ibadani, michezoni, misibani maana huko kote kuna mikusanyiko ya watu zaidi ya 19 na hivyo inaweza kuhesabika kama "Unlawful assemly".

2. Hao vijana walipokamatwa hawakuwa na silaha yoyote hata Fimbo. Sasa unawezaje kusema mkusanyiko wa vijana hao unatishia amani wakati hawana silaha yoyote?

3. Nilipokua chuoni "group discusion" yangu ilikua na watu 20. Ina maana na sisi tungekusanyika nje ya chuo kujadili mambo ya kitaaluma tungeambiwa "Unlawful Assembly?", tungeambiwa tunatishia amani?

4. Polisi watueleze mikusanyiko isiyotishia amani inapaswa kuwa na watu wangapi?

5. Nina ratiba ya kwenda kumsalimia pacha wangu Manawa Bukwimba mwezi ujao. Huyu jamaa ana familia kubwa sana, hivyo natarajia kupokewa na watu zaidi ya 50. Je Polisi watatukamata kwa kufanya kusanyiko lisilo halali?

6. Polisi wameanza lini kuhukumu watu kwa hisia? Kwa mujibu wa hati ya mashtaka vijana waliokamatwa wanadaiwa kuwa walitaka kuandamana. How can u prove their intention? Eti Polisi wanahisi walitaka kuandamana. Kwa hiyo Polisi wakihisi nataka kumuacha mke wangu wataniletea talaka nyumbani?

7. Kwanini Polisi hawakukamata wafuasi wa CCM walioandamana juzi bila kibali, wanakimbilia kukamata vijana ambao hawajaandamana ila wanawahisi eti walitaka kuandamana.?

8. Kauli aliyoitoa Masha kwa Polisi inafanana na kauli aliyoitoa Rais Mkapa kwa Watanzania. Masha anadaiwa kuwaita Polisi wapumbavu, Mkapa nae aliwaita watanzania wapumbavu. Mbona Mkapa hakushtakiwa?

9. Masha amesema Polisi hawana dini wala hawana huruma. Je ni uongo? Polisi wangekua na dini na moyo wa huruma wangemuua Mwangosi kama Mbwa? Wangewapiga risasi wafuasi wa vyama vya siasa wanaoandamana kwa amani? Wangewaua wale wafanyabiashara wa Kilosa kwa kuwapiga risasi ili wachukue fedha zao?

10. Ikiwa Polisi wameweza kutenda ukatili huu kwa mtu aliyewahi kuwa "boss" wao (waziri wa mambo ya ndani), vp kwa wananchi wa kawaida? Kama Waziri anabambikiziwa kesi, mwananchi mnyonge itakuaje?

#MWISHO_WA_UONEVU_NI_OCTOBER_25



No comments: