Monday 21 September 2015

NAANDIKA kujibu makala ya Dk. Hamisi Kigwangalla iliyochapishwa katika gazeti hili, toleo namba 421 la Septemba 2-8,2 015 ukurasa wa 27, yenye kichwa cha habari “Tutimize wajibu wetu 2015”
Lengo la makala hii ni kuweka sawa upotoshaji wa makusudi au kuziba nakisi ya kiweledi iliyojitokeza katika makala ya mwanasiasa huyu msomi kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa faida ya wasomaji wa gazeti hili na Watanzania kwa ujumla, hasa katika kipindi hiki ambacho Watanzania wanakabiliwa na mtihani wa kiuamuzi kupitia nguvu yao ya sanduku la kura
Kwanza naomba nikubaliane nae kuwa Chama Cha Mapinduzi kimegusa kwa namna moja au nyingine maisha ya Watanzania wote katika nyakati mbalimbali. Kuna walioguswa nacho katika hali chanya na wengine hali hasi.`
Lakini vile vile mwandishi wa makala hiyo katika aya ya tatu anaandika kuwa kuna Watanzania waliosomeshwa bure na Serikali ya CCM na wengine kupewa uhuru wa kuanzisha vyama vya siasa na sasa wanaitukana serikali kwa uhuru uliopitiliza.
Pengine mwandishi huyu pamoja na kuwa msomi wa kiwango kikubwa na mwanasiasa mzoefu, bado anahitaji elimu ya uraia (Civic Education). Ni jambo la kushangaza kuwa bado kuna watu wanaamini kuwa Serikali ya CCM haipaswi kukosolewa eti kwa sababu ilikusomesha bure. Hizo fedha za kusomesha bure Serikali ya CCM ilizitoa wapi? Serikali ya CCM ilisomesha bure tena sio CCM hii bali ile CCM ya Mwalimu Julius Nyerere, ambaye kwa uzalendo na mapenzi yake kwa Tanzania aliamua kuwasomesha bure vijana ili baadaye waje kulitumikia taifa lao na sio kukitumikia chama na kukiimbia nyimbo za sifa na kukitukuza hata pale kinapoonekana kinapoteza mwelekeo. Sifa kuu ya msomi ni kutoa mawazo huru na kutoa mwelekeo sahihi wa dira (vision) na dhima (mission) kwa taasisi au jamii fulani ili kufikia malengo mapana iliyojiwekea.
Lengo la Serikali ya Mwalimu Nyerere kusomesha bure tena kwa kutumia Kahawa, Mkonge na Pamba lilikuwa kuhakikisha kuwa anajenga taifa linalojitosheleza kwa rasilimali, hasa rasilimali watu kwani elimu ndio kipaumbele cha msingi kabisa kwa taifa lolote linalopenda kupiga hatua.

Cha ajabu baadhi ya wasomi hao ndio waliokuja kugeuka jeshi la maangamizi kwa taifa hili na kujenga himaya kubwa ya mafisadi ambao wanaliibia taifa na kutukuza kila aina ya uzembe na unyonyaji kwa Watanzania wenzao, kiasi cha kulirudisha taifa nyuma na kisha taifa letu kupoteza mwelekeo.
Nasikitika kusema kuwa mwandishi wa makala ile naye ameingia moja kwa moja katika kundi hili ndio maana anashangaa kuwa baadhi ya watu waliosomeshwa bure kwa nini wanakikosoa Chama Cha Mapinduzi na serikali yake (yeye anatumia neno kutukana). Kama wasomi hawawezi kuona mwelekeo mbaya wa jamii au taasisi zao na taifa kwa ujumla na kisha kuchukua hatua basi ni afadhali watu hao wasingeuona mlango wa darasa kabisa
Katika aya ya tano mwandishi anasema; “CCM ilitanua demokrasia na kuruhusu mfumo wa vyama vingi.” Kwa mwanafunzi wa darasa la tano ambaye amesoma vizuri Somo la Uraia na pia mwanafunzi mzuri wa Somo la Historia hapaswi kusubiri hadi ahitimu Shule ya Msingi na kufikia kiwango cha Shahada ya Uzamili ili afahamu kuwa nchi yetu ilipita katika histori ya mfumo wa vyama vingi hata kabla ya Uhuru ambapo chama cha TANU ambacho kilikuja kushirikiana na chama cha ASP, kilishindana na vyama vingine kwenye uchaguzi. Mfumo wa vyama vingi umekuwapo kabla hatujapata Uhuru lakini ulikuja kunyongwa baada ya sisi kupata Uhuru wa bendera kutoka kwa wakoloni.
Kwa mfano Zanzibar kulikuwa na vyama kama Zanzibar National Party (ZNP) kilichoanzishwa mwaka 1955, kisha Afro-Shiraz Party (ASP) mwaka 1957 chini ya Abeid Amani Karume, pia Zanzibar and Pemba People’s Party (ZPPP) mwaka 1959 chini ya uongozi wa Sheikh Muhamed Shamte na pia Chama cha Umma yaani “Umma Party’ mwaka 1963, chini ya Abdulrahaman Mohamed Babu. Kwa upande wa Tanganyika kulikua na vyama kama Tanganyika United Party (UTP), African National Congress (ANC) na African Muslims National Union of Tanganyika (AMNUT).
Kwa hiyo mfumo wa vyama vingi ulikuwapo hadi ulipokuja kufutwa na serikali za chama cha TANU na ASP. Si kweli kwamba CCM inastahili kupewa sifa za kupanua demokrasia bali chenyewe kina unasaba na vyama vilivyonyonga demokrasia baada ya Uhuru na kisha baadaye kuja kuruhusu mfumo wa vyama vingi kwa shingo upande baada ya shinikizo la kiharakati na ndiyo maana baada ya kuruhusu mfumo huo wa vyama vingi kwa shinikizo la kisiasa na kiuchumi kutoka ndani ya nchi na jumuiya ya kimataifa kiasi cha kwenda kinyume na hiyo asilimia 80 iliyopiga kura ya maoni kutaka mfumo wa chama dola uendelee, bado waliendelea kubadili mfumo kinyume cha matakwa ya wengi (Kwa uzoefu ule ule wa kufanya uamuzi kidikteta) lakini pia wakashindwa kuweka uwanja sawa wa kufanya siasa ili kuirutubisha demokrasia.
CCM wangekua wapenda demokrasia kweli wangekubali kubadili tume ya uchaguzi na kuweka tume huru ya uchaguzi, watumishi wa serikali kama wakuu wa wilaya na mikoa wasingepaswa kuwa wajumbe wa vikao vya CCM kama ilivyo ambapo wakuu wa wilaya ni wajumbe wa kamati za siasa za wilaya na wakuu wa mikoa halikadhalika.
CCM hiyo inayopenda demokrasia isingechakachua maoni ya wananchi na kutumia Bunge la Katiba kama chombo cha kunyongea demokrasia na kuvisha kitanzi maoni ya wananchi.
Kwa hiyo Serikali ya Chama cha Mapinduzi haina historia ya kukubali siasa za ushindani, bali ilishiriki kwa hila kunyonga demokrasia. Historia inatuonyesha hivyo.
Katika aya ya sita ameendelea kufanya kosa lile kwa makusudi au kwa kutoelewa anapoendelea kuhalalisha upotoshaji huo kwa kujenga hoja kuwa; “Bila CCM madhubuti nchi yetu itayumba.” Kwanza msingi wa kauli hii ni kutokana na mawaidha ya Mwalimu Nyerere aliyoyatoa enzi za mfumo wa chama kimoja yaani CCM ikiwa Chama Dola (State Party). Kwa wakati ule ilikuwa sahihi kwa Mwalimu kutoa tahadhari ile kwani huwezi kuwa na chama dola legelege huku ukitarajia kuwa na serikali imara au taifa imara.
Ni lazima nchi itayumba, taifa litayumba. Na hii ndio hatari kubwa inayoyakabili mataifa yanayoendeshwa kwa mfumo wa vyama Dola. Kwa mfano leo Chama cha Kikomunisti cha China (CCP) kikiyumba na taifa la China litayumba. Huwezi kukiathiri chama dola bila kuathiri serikali kwani chama ndio serikali na serikali ndio chama.
Sasa nashangaa msomi huyu kutoa mawazo haya leo katika enzi za mfumo wa vyama vingi, hata Mwalimu angekua hai leo angemshangaa msomi huyu na ndio maana baada ya mfumo wa vyama vingi kuruhusiwa Mwalimu alibadili mtazamo wake na kudai “Watanzania wanataka mabadiliko, wasipoyaona, wasipoyapata ndani ya CCM basi watayatafuta nje ya CCM”.
Kwa hiyo aliwaasa waachane na ile kasumba chafu kuwa bila CCM madhubuti (CCM Dola), nchi itayumba. Alitaka wajitambue kuwa sasa kuna mfumo wa vyama vingi hivyo chama kikubali kukosolewa na kijirekibishe ili kifanye uamuzi sahihi na makini zaidi
Sote tunajua kwamba demokrasia ya vyama vingi inastawi pale nchi inapokuwa na uwanja wa ushindani ulio sawa (level playing field).
Mwaka 1991, Tume ya Jaji Francis Nyalali iliyopendekeza kurudishwa kwa mfumo wa demokrasia ya vyama vingi ilipendekeza pia, kupitia taarifa yake iliyokuwa na vitabu (volumes) vitatu, haja ya kwanza kubadilisha Katiba, sheria na misingi ya utawala katika maeneo mengi ili kuondoa nafasi ya CCM kudhibiti hatamu zote na pia kudhibiti taasisi zote kuu za nchi pamoja na rasilimali nyingi ambazo kimsingi zilipatikana kupitia michango ya lazima iliyokamuliwa kwa wananchi ambao wengi wao hawakuwa hata wanachama wa CCM.
Kwa muhtasari ni kwamba Tume ya Nyalali ilitaka kwanza CCM kiondolewe nguvu hizo kubwa ambazo haikuzipata kutokana na kazi ya kisiasa iliyofanya au kukubaliwa kwake kwa hiyari na wananchi bali kutokana na kuhodhi kwake kwa mabavu mamlaka makubwa chini ya dhana ya "Chama kushika hatamu" (Party Supremacy), dhana iliyokifanya kisiwe chama cha siasa bali ni chama dola (state party) ambacho kilikuwa siyo tu chama pekee cha siasa lakini zaidi ili kukiweka juu ya mamlaka na taasisi nyingine zote za dola tena kwa mujibu wa Katiba na sheria za nchi.
Kwa kutumia dhana hiyo ya "Chama kushika hatamu" (Party Supremacy), Katiba na sheria za nchi ziliiweka CCM kuwa juu ya serikali, Bunge, Mahakama na hata vyombo vya ulinzi na usalama. Tume ya Nyalali kwa usahihi kabisa iliona hali hiyo itaondoa kabisa dhana nzima na maana ya kuruhusu demokrasia ya vyama vingi nchini na itasababisha CCM kuwa juu ya vyama vingine si kwa sababu ya kukubalika kwake na wananchi bali kwa sababu ya mfumo wa kikatiba, kisheria na utawala unaokilinda.
Pia mwandishi ameendelea kujenga hoja kuwa “vyama vya upinzani ni vichanga na haviwezi kuaminiwa kwa kuwa vinahitaji kukua kiitikadi, kumuundo na kisera.” Mwandishi amejenga hoja dhaifu sana isiyozingatia utafiti wa kisomi. Hapa kwa majirani zetu Kenya, Muungano wa JUBILEE uliowaingiza madarakani Rais Uhuru Kenyatta na Naibu wake William Ruto ulijengwa juu ya misingi ya vyama viwili vichanga vya TNA na URP. Kule nchini Zambia chama tawala cha UNIP kiliondolewa madarakani na chama kipya cha MMD kilichoasisiwa takribani mwaka mmoja kabla ya uchaguzi. Hii ilitokana na mgawanyiko pia uliotokea ndani ya chama cha tawala na kuunda chama kingine cha upinzani chenye nguvu ambacho kilikiondoa chama tawala kwa sababu umma ulitaka mabadiliko na Rais Kenneth Kaunda alikabidhi madaraka kwa amani (peaceful transition). Tukisalia hapo hapo Zambia utaona kuwa wananchi walikuja kukiondoa madarakani chama cha MMD mwaka 2011 na kukikabidhi madaraka chama cha Patriotic Front kilichoasisiwa miaka 10 kabla ya uchaguzi.
Michael Satta alishinda uchaguzi kwa kuwa umma ulihitaji mabadiliko na kwa kuwa waliridhishwa na ajenda za chama cha upinzani. Hapa kwetu Tanzania vyama vinavyounda Ukawa yaani Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi na NLD vina umri wa miaka takribani 23 sasa.
Baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010, Chadema kilijenga mfumo thabiti hadi kwa ngazi za chini kupitia programu ya Chadema ni msingi. Ngazi ya misingi kwa Chadema inashabihiana na ngazi ya shina kwa upande wa CCM. Ni muundo huu uliosaidia kukitikisa chama tawala katika misingi yake katika uchaguzi wa serikali za mitaa mwaka jana na kuporomosha vibaya ushindi wa CCM kilichokuwa kikishinda uchaguzi wa serikali za mitaa kwa asilimia 98 miaka ya nyuma.
Mwandishi anaendelea kusema kwamba upinzani hauna uthabiti katika itikadi na sera. Chadema kimejipambanua kabisa kisera na kiitikadi. Chadema ni chama cha mrengo wa kati ambacho katika kukuza uchumi Serikali ya Chadema itabadili mfumo wa uchumi ili kuhakikisha mfumo huo unajengwa katika mfumo utakaoifanya nguvu ya soko kutumikia jamii ambao unatambulika kama ‘Social Market Economy’. Kazi ya serikali ya itakayoundwa na Chadema na kuungwa mkono na vyama washirika wa Ukawa itakuwa ni kuweka uwiano wa mapato utakaohakikisha huduma za kijamii zinapatikana kwa urahisi na kwa ufanisi.
Ndiyo maana katika ilani ya uchaguzi ya Chadema inayoungwa na Ukawa imeweka msimamo wake wazi kwenye masuala ya elimu na afya. Kwenye afya, serikali itahakikisha kuwa inagharamiwa kwa bima ya gharama nafuu na mifuko ya hifadhi ya jamii. Pia afya ya msingi na kinga itaimarishwa ili kupunguza gharama za matibabu. Mfumo wa soko-kijamii (Social Market) kama ilivyo sera ya uchumi ya Chadema katika afya utahakikisha gharama za matibabu zinadhibitiwa bila kuathiri uendeshaji wa watoaji wa huduma za afya kama vile hospitali za serikali na zile za sekta binafsi. Si lengo la makala hii kujadili kwa kina kuhusu “social market Economy”, nitaeleza kwa undani kuhusu mfumo huu siku zijazo.
Namshangaa Dk. Kigwangalla kujadili suala la itikadi kwa vyama vya upinzani wakati anajua kuwa chama chake pamoja na ukongwe wake hakina itikadi. Ukisoma Katiba ya CCM utaona kwamba chama hicho kinajiita chama cha kijamaa (Socialist Party) na pia Serikali ya CCM waliporekebisha Katiba ya nchi mwaka 1977 wameendelea kuitambulisha Tanzania kama dola ya kijamaa (Socialist State) lakini mfumo wa CCM unaendeshwa kibepari na pia nchi inaendeshwa kibepari kama alivyokiri kuwa tunafuata mfumo wa soko huria (Free Market). Kwa nchi kama Tanzania ambayo Mwalimu Nyerere aliweka misingi ya kijamaa kuja kubadilisha kwa azimio la pupa ‘Azimio la Zanzibar’ na kuingia katika Soko Huria (Isomeke Soko Holela) ambalo hadi huduma muhimu kama elimu, afya na hata ‘’kiu” (huduma ya maji) imewekwa katika soko na kudalaliwa kibepari ni hatari sana. Serikali inapoacha nguvu ya soko pekee bila kuweka uwiano wa mapato ili kuhakikisha huduma za kijamii zinapatikana kwa ufanisi ni jambo hatari kwa nchi masikini kama Tanzania.
Zaidi ya asilimia 70 ya Watanzania kwa sasa hawapati huduma za kijamii kwa ufanisi kutokana na serikali kurukia mfumo wa soko huria bila kuweka misingi ya kuliandaa taifa kimfumo. Hii yote ni kutokana na ombwe la kiitikadi ambalo CCM ilianza kuonyesha na kusababisha ombwe kubwa katika uongozi wa nchi.
Ni hatari zaidi kuwa na chama cha siasa madarakani ambacho hakifuati itikadi yake au hakina itikadi kabisa. Ndio maana Serikali ya CCM imekua bingwa wa kurukia sera za vyama vingine kama sera mpya ya elimu ya serikali iliyozinduliwa na Rais Jakaya Kikwete ni nakala ya sera yetu ambayo tuliizindua kwenye mkutano mkuu wa Septemba 2014. Kwa hiyo hadi sasa Dk. Kigwangalla ni kwamba, aidha alikua hajui alichokuwa anahubiri, hakijui chama chake vizuri, alifanya upotoshaji wa makusudi au vyote kwa pamoja.
Inashangaza kuona msomi anayejivunia kusomeshwa bure na Serikali ya CCM anapokisifia chama asichojua hata itikadi yake na wala sera zake. Ni katika mazingira haya ndipo unapokutana na mambo ya ajabu kabisa katika ilani ambayo inajadili suala la kufufua viwanda utadhani kulikua na chama kingine tofauti madarakani kilichoshindwa kusimamia uwekezaji na kupelekea viwanda kufa.
Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya 2015 – 2020, chama kinachotawala na kinachotaka kiendelee kutawala hakiongelei chochote juu ya ilani iliyopita, jinsi ilivyopaswa kutekelezwa, wapi ilifanikiwa na wapi haikufanikiwa na haielezei ni kwa nini haikufanikiwa na badala yake CCM wanakuja na ilani mpya ya moja kwa moja, utadhani wanataka kuingia madarakani kwa mara ya kwanza.
Katika ilani yao CCM wanasema kuwa chini ya utawala wao Watanzania wamepata mafanikio makubwa ya kiuchumi, kisiasa na kijamii, lakini hawajatuambia haya mafanikio ni makubwa kulinganisha na yapi, yaliyopita? Yaliyotarajiwa au inavyopaswa kuwa kwa mtizamo wao?
Katika ilani yao, bado wanagusia kupunguza tatizo la ajira na hasa kwa vijana. Hapa wameshashindwa kuondoa tatizo hilo kabla ya kuanza kutekeleza ilani yao maana wanaongelea kupunguza badala ya kulimaliza kabisa ili kama ikitokea wakashindwa kulimaliza, basi watalipunguza kwa kiasi kikubwa. Sasa kama lengo ni kupunguza, basi wakishindwa litapungua kwa kiasi kidogo tu. Na wanaongelea kupunguza tatizo hili la ajira kwa vijana pekee na sio rika lingine la Watanzania.
Ilani ya CCM inaongelea juu ya kuwawezesha wafanyabiashara wadogo kupata mikopo nafuu na kuwapatia maeneo ya kudumu ya kufanyia biashara zao. Hapa kwanza ilani ya chama kinachotawala itueleze kwanza ni kwa nini imekuwa ikiwafukuza na kuwanyang’anya vitendea kazi pamoja na bidhaa zao hawa wafanyabiashara wadogo katika miji yetu, na ni kwa nini sasa inafikiri ni wakati wa kuwatambua hawa wafanyabiashara, maeneo mazuri ya kufanyia biashara na kuhakikisha wanapata mikopo nafuu na ni kwa nini haipangi kuwawezesha hata ikibidi kwa kuwapa ruzuku wafanyabiashara hawa ili wawe wafanyabisahara wakubwa na ikibidi wakatafute masoko nje ya nchi.
Mgombea wao wa urais anapoahidi kuanzisha Mahakama Maalumu (Special Tribunal) ya kupambana na rushwa inamaana kwamba kwa mtazamo wa wasomi hawa, tatizo la rushwa ni kwa sababu mahakama hazitoshi? Kama kungekuwa na nia ya dhati katika hili Serikali ya CCM ilipaswa kuonyesha nia hiyo kwa kuifanya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) inakuwa huru (Independent).
Kwa kuanza ilipaswa uteuzi wa mkurugenzi mkuu wake uthibitishwe na Bunge. Leo Rais ambaye ni mwenyekiti wa CCM anapomteua Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru bila kuhojiwa na chombo chochote unadhani mkurugenzi na watendaji wa Takukuru waliopo chini yake watafanya kazi kwa uhuru? Ndio maana baadhi ya maofisa wa Takukuru walipomkamata kiongozi mmoja wa ngazi ya juu ya CCM wakati wa mchakato wa kura ya maoni walimuachia katika mazingira tata. Wangemfanya nini wakati kwa kufanya hivyo wangekua wanamuathiri Mwenyekiti wa CCM ngazi ya taifa, ambaye ndiye aliyemteua Bosi wao wa Takukuru?
Kuanzisha Mahakama Maalumu bila maandalizi ya kubadili fikra za viongozi na taifa kwa ujumla kwa kuzingatia tunu zilizopendekezwa kwenye rasimu ya Katiba ya wananchi hakutasaidia lolote. Matokeo yake hata majaji wa Mahakama hiyo watajikuta nao wakitakiwa kukamatwa na kushtakiwa kwa tuhuma za rushwa kama inavyotokea kule Indonesia ambako hadi Jaji Mkuu, Akil Mochtar, alijikuta anashtakiwa kwa rushwa
Haya machache niliyoandika yatoshe kidogo kupunguza upotoshaji ambao umekuwa ukifanywa na mwandishi. Naomba nimalizie kwa kutoa rai kwa Dk. Kigwangalla kuwa CCM ya sasa ina ombwe la kiitikadi na serikali yake imepoteza mwelekeo kisera. Ni bora ajielimishe zaidi kwenye masuala ya itikadi na sera kabla
hajachukua kalamu na kuandika kipindi kingine ili asijikute anakivua nguo chama chake na serikali yake kama alivyofanya katika makala zake zilizopita
Chama Cha Mapinduzi kimekuwa na wafuasi na wanachama watiifu na kujijengea tanzi tiifu (Loyal Base) kubwa lakini tanzi shabiki (fan base) ndogo huku upinzani ukiwa na tanzi tiifu ndogo lakini tanzi shabiki kubwa zaidi. Tangu kumalizika kwa uchaguzi wa mwaka 2010, upinzani uliweza kuweka mkakati wa kuifanya tanzi shabiki yake kubwa kuwa tanzi tiifu kwa mabadiliko kutokana na mikakati ya upinzani ndani na nje ya Bunge, hatua za kiharakati na kisiasa na pia makosa mengi ya CCM ambacho kilizidi kujiharibia kwa kudandia hoja za upinzani kama ile ya Katiba mpya ambayo tayari umma ulishakua na kiu nayo. Walipodandia na kuharibu kwa makusudi mchakato ule wakajikuta wanakasirisha wananchi huku upinzani ukitumia fursa hiyo kuungana na kujaza wananchi matumaini makubwa ambayo hawajawahi kuwa nayo katika historia ya mfumo wa vyama vingi.
Hila za CCM zilisababisha matokeo chanya ya kuunganisha wapinzani na kuzalisha Ukawa. Hila hizo hizo wakazirudisha ndani na kugeuziana kibao katika mchakato wa uteuzi ndani ya chama kwa kuwa walishazoea mizengwe. Wakajikuta wamewafanyia hila wana-CCM watiifu na mashabiki kwa kumkata kimizengwe mgombea aliyekuwa akipendwa na wananchi wengi na wanachama wengi zaidi wa CCM. Ukawa ikapata silaha nyingine Edward Lowassa
Upinzani tunapita katika historia nyingine inayofanana na historia ya vyama vya MMD kilichokiondoa chama tawala cha UNIP ya Zambia, Kama historia ya NAARC kilichokiondoa chama cha KANU kule Kenya. Tumeweza kufikia hatua hii ya juu baada ya kutimiza vigezo muhimu yaani kwa chama tawala kugawanyika kama ilivyogawanyika KANU na UNIP kule Kenya na Zambia mtaalia (respectively) na pia hatua muhimu zaidi ya upinzani kuungana na mwisho kabisa kuwa na ajenda ambazo wananchi wamezikubali na kuzipokea. Muhimu kwa sasa ni chama tawala kianze kufanya maandalizi ya kuwa chama cha upinzani
Kwa sababu ya nafasi ninaomba kuishia hapa kwa sasa. Natarajia kuandika kwa kina kujibu swali la mwandishi wa makala ile alilouliza wapinzani wana jipya?
Mwandishi wa makala hii Ben-Rabiu Saanane ni Mkuu wa Idara ya Sera na Utafiti ya Chadema. Ni mwanasiasa, msomi mwenye shahada ya kwanza ya biashara (BBA Hons), shahada ya uzamili katika uchumi na shahada ya uzamili katika uhusiano wa kimataifa na diplomasia. Kwa sasa ni mwanafunzi wa shahada ya uzamivu (Ph.D in Governance and Policy Analysis). Anapatikana kwa simu 0768078523
-

No comments: