Saturday 11 January 2014

UZINDUZI WA KITABU CHA HISTORIA YA ZANZIBAR MIAKA HAMSINI YA MAPINDUZI

  Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad na Rais Mstaafu Dkt. Amani Abeid Karume, wakionyesha kitabu cha Picha za historia ya Zanzibar, baada ya kukizindua huko Makumbusho ya Mnazi mmoja.


 Mtunzi wa kitabu cha Picha za historia ya Zanzibar Bw. Javed Jafferji, akitoa ufafanuzi wa kitabu hicho kabla ya kuzinduliwa rasmi.
 Baadhi ya mashuhuda katika uzinduzi wa kitabu cha Picha za historia ya Zanzibar,hafla iliyofanyika Makumbusho ya Mnazi mmoja.
 Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, akisalimiana na mke wa muasisi wa Mapinduzi Mama Fatma Karume wakati wa hafla ya uzinduzi wa  kitabu cha Picha za historia ya Zanzibar kwa miaka 50 ya Mapinduzi.
Waziri wa Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo Mhe. Said Ali Mbarouk, akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa kitabu cha Picha za historia ya Zanzibar kwa miaka 50 ya Mapinduzi. (picha na Ali Hamad, OMKR).

Na Hassan HAmad OMKR
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, amesisitiza haja ya kuendelezwa vipaji vya uandishi wa vitabu, ili kuwasaidia wananchi kujua mambo mbali mbali yakiwemo ya kihistoria.
Mhe. Maalim Seif ametoa wito huo katika viwanja vya makumbusho ya Mnazi mmoja, wakati akizindua kitabu cha Picha za historia ya Miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar, kilichoandikwa na mwandishi mzalendo Bw. Javed Jafferji.
Amesema iwapo vipaji vya aina hiyo vitaendelezwa, vitaweza kuibua vipaji vyengine zaidi ambavyo vitapelekea kuitangaza Zanzibar na wazanzibari, sambamba na kuendeleza kasi ya kukuza uchumi.
Amesema kitabu hicho ni muhimu kwa Zanzibar, kwani kimeelezea nyanja mbali mbali za maendeleo ikiwa ni pamoja na sekta ya utalii ambayo ndio sekta kiongozi kwa uchumi wa Zanzibar.
Akizungumzia kuhusu miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar Mhe. Maalim Seif amewakumbusha wazanzibari kuendeleza amani na umoja, ikiwa ni njia moja wapo ya kumuenzi marehemu Mzee Karume na kuendeleza malengo ya Mapinduzi.
Amesema Mzee Karume alikuwa mstari wa mbele katika kuhimiza umoja na maelewano miongoni kwa wananchi, na kwamba ndio msingi wa maendeleo kwa nchi yoyote duniani.
Amefahamisha kuwa sherehe za miaka 50 ya Mapinduzi zimekwenda sambamba na historia ya Mapinduzi yenyewe ambayo yalifanyika siku ya Jumamosi kuamkia Jumapili kama ilivyo kilele cha maadhimisho hayo mwaka huu.
Maalim Seif ambaye ameshiriki katika kitabu hicho kwa kuandika Utangulizi ambapo Rais Mstaafu Dkt. Amani Abeid Karume naye alishiriki kwa kuandika dibaji ya kitabu, amesifu kazi kubwa iliyofanywa na mwandishi huyo ya kukusanya picha muhimu za kihistoria ambazo baadhi yake ni adimu kwa wazanzibari.
Kwa upande wake Rais mstaafu wa awamu ya sita Mhe. Dkt
Amani Abeid Karume amesema kitabu hicho kinaendeleza historia ya Mapinduzi ya mwaka 1964.
Amesema lengo la Mapinduzi ni maendeleo kwa wazanzibari wote,
na kwamba Wazanzibari wote ni wanamapinduzi na waumini wa Mapinduzi hayo kulingana na historia ya nchi ilivyo.
Mapema mwandishi wa kitabu hicho Bw. Javed Jafferji amesema kitabu hicho kilichomchukua muda wa mwaka mmoja hadi kukamilika kwake, kimekusanya matukio ya kihistoria yakiwemo historia za watu mashuhuri.
Amesema alishajiika kuandika kitabu hicho baada ya kuona kinakidhi haja  ya kihistoria kwa miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Naye Waziri wa Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo Mhe. Said Ali Mbarouk amesema kitabu hicho kitakuwa chachu ya mafanikio katika nyanja mbali mbali ikiwemo Utalii.
Amesema mwandishi wa kitabu hicho amekuwa mshirika mkubwa wa Wizara ya Habari, na kwamba wataendelea kushirikiana nae katika kazi zake ili aweze kuchangia maendeleo ya Zanzibar kupitia taaluma hiyo ya uandihsi.
Uzinduzi huo wa kitabu umekwenda sambamba na maonyesho ya picha za kitabu hicho ambazo zitakuwepo katika makumbusho ya Mnazi Mmoja, na kuwataka wananchi kutembelea makumbusho hayo kwa lengo la kujifunza.

No comments: