Friday 27 March 2015

Ofisi ya CUF Z’bar yateketea kwa moto

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi Kamanda Mkadam Khamis
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi, Mkadam Khamis Kmadam
Ofisi za jengo la tawi la Chama cha Wananchi (CUF) Jimbo la Dimani, mkoa wa Mjini Magharibi, limeteketea kwa moto na kusababisha hasara kubwa ya vitu vilivyokuwamo humo ingawa thamani ya vitu hivyo haijajulikana.
Tukio hilo lilitokea mtaa wa Kisauni usiku wa kuamkia jana saa nane usiku.
Mashuhuda walisema watu wasiojulikana walifika na gari aina ya Pick-up na kuvunja mlango wa ofisi hizo na kulilipua jengo hilo kwa petroli.
“Majira ya saa nane usiku ilikuja gari na watu wawili walishuka katika gari hiyo na kuingia ndani huku wakisikika wakisema tayari tuondoke na baada ya kuondoka tu jengo hilo lililipuka,” alisema shuhuda mmoja aliyekuwapo katika eneo hilo.
Alisema baada ya kuona moto na moshi mkubwa ukiwa umetanda ndipo walipowapigia watu wa Zima Moto na walifika kuuzima.
Diwani wa wadi ya Tomondo, Hassan Hussen Yussuf, alisema hali inasikitisha katika harakati za kisiasa kuona Zanzibar inarejea katika siasa za chuki na uhasama.
“Matukio kama haya hutokea karibu na uchaguzi kwa kweli inasikitisha sana na kama halii itaendelea itakuwa hatari katika nchi,” alisema Yussuf.
Alisema katika jengo hilo kulikuwa na vifaa mbalimbali vya thamani na fedha taslimu za malipo ya uchukuaji wa fomu za wagombea walizolipia zimeteketea.
Mkurugenzi wa Haki za Binadamu na Mawasiliano ya Umma wa CUF, Salum Bimani, alisema CUF kinalihusisha tukio hilo kuwa ni joto la uchaguzi na kuwashutumu waliofanya waliofanya tukio hilo kwani matukio kama hayo yamekuwa yakifanywa inapokaribia kipindi cha uchaguzi mkuu.
“Hujuma hizi zimepangwa na ni za makusudi kuchafua amani ya nchi, na hali kama hii hutokea zaidi karibu na uchaguzi na CUF hufanyiwa hujuma mbalimbali ikiwamo kuchomwa moto ofisi zetu,” alisema Bimani.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Mjini Magharibi, Mkadam Khamis Mkadam, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema kuwa Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi.
Chanzo: Nipashe

No comments: