Tuesday 15 December 2015

Marekani yamuweka Magufuli njiapanda


Marekani imeiweka njiapanda Serikali ya Rais Dk. John Magufuli, baada ya Bodi ya shirika lake la Changamoto za Milenia (MCC) kuamua kukutana kesho kujadili masuala kadhaa ya utoaji wa misaada kwa nchi zinazoendelea huku angalizo lake kwa serikali ya Tanzania kuhusiana na uchaguzi wa Zanzibar likiwa bado halijapatiwa ufumbuzi.

Rais Dk. John Magufuli

Kwa mujibu wa ratiba ya MCC, kikao chao cha Bodi kitakutana kesho (Jumatano) na kupitia mapendekezo ya kupeleka misaada kwa nchi mbalimbali zinazoendelea. Inaelezwa kuwa kikao hicho kitafanyika kwenye ukumbi wa Holbrooke, saa 4:00 asubuhi kwa saa za Marekani.

Inatarajiwa kuwa kupitia kikao hicho, nchi zitakazokidhi vigezo zitakuwa na fursa ya kuidhinishiwa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo iliyojipangia yenyewe kabla ya kupata fedha hizo. Tanzania inasubiri kuidhinishiwa fedha za awamu ya pili za MCC Dola za Marekani milioni 472 (takribani trilioni moja).

Hata hivyo, kutokana na ratiba hiyo, Serikali ya Rais Magufuli inatarajiwa kuwa njiapanda kwani suala la Zanzibar lililokumbushiwa na MCC kupitia maelekezo yake yaliyoripotiwa mwezi uliopita, bado linaonekana kuwa kuendelea kuwa tete. Hadi sasa, licha ya vikao mbalimbali vinavyoendelea kufanyika na kuwakutanisha wagombea waliokuwa wakichuana kwa karibu kabla ya uchaguzi huo kufutwa, Dk. Ali Mohamed Shein wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Maalim Seif Shariff Hamad wa Chama cha Wananchi (CUF), bado ufumbuzi haujapatikana.

CCM wanaamini kuwa uchaguzi huo ni lazima urudiwe baada ya kufutwa na Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), Jecha Salim Jecha, huku CUF wakisisitiza kuwa uchaguzi huo haukuwa na kasoro kubwa kiasi cha kufutwa wote na hivyo kutaka matokeo yatolewe na mshindi atangazwe kuwa Rais wa visiwa hivyo.

Awali, katika angalizo lake kwa serikali ya Magufuli iliyoingia madarakani Novemba 5, 2015, MCC ilitaka kupatiwa ufumbuzi kwa suala la Zanzibar na pia kuwapo kwa ufafanuzi juu ya watuhumiwa waliokamatwa kwa makosa ya mtandao wakati wa Uchaguzi Mkuu, Oktoba 25.


Ilifahamika kuwa maelekezo ya MCC kwenda kwa mamlaka mbalimbali za serikali ya Tanzania, yalionyesha kuwa lipo tishio la kufutwa kwa msaada huo (trilioni moja) iwapo mgogoro wa kisiasa wa Zanzibar hautapatiwa ufumbuzi na pia kutolewa ufafanuzi wa sheria ya makosa ya mtandaoni kabla ya kikao cha bodi ya MCC mwezi huu (Desemba, 2015).

“MCC inafuatilia kwa karibu hatua zitakazochukuliwa na serikali ya Magufuli katika suala la utawala bora, katika kipindi hiki tunapokaribia kufanya kikao cha bodi ya MCC Desemba. Utatuzi wa mgogoro wa Zanzibar kwa kuridhisha pande zote zinazohusika,” ilielezwa katika kile kilichodaiwa kuwa ni sehemu ya angalizo la MCC kwa serikali ya Tanzania na kuripotiwa Novemba, 2015.

Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue, aliwahi kulitolea ufafanuzi suala hilo alipozungumza na gazeti hili Novemba 29, 2015, akisema kuwa Serikali haina wasiwasi kuhusu mashariti ya MCC juu ya Zanzibar kwani yatafanyiwa kazi kabla ya bodi ya MCC kukutana tena (Desemba).

Hata hivyo, hadi sasa hakuna muafaka uliotangazwa rasmi kuwa umefikiwa kuhusiana na uchaguzi wa Zanzibar huku pande zote zikiendelea kutoa msimamo tofauti; hali hiyo ikielezwa kuwa inaiweka njia panda serikali ya Magufuli kwani fedha za MCC ni muhimu katika utekelezaji wa ahadi zake mbalimbali, hasa juu ya dhamira ya kusambaza umeme na kuwaunganisha wananchi wengi katika gridi ya taifa.

Kadhalika, fedha za awamu ya pili za MCC ni muhimu pia katika uimarishaji wa taasisi zinazohusika na sekta ya nishati.

Akizungumzia hatari iliyopo sasa ya kukosa fedha za MCC baada ya suala la uchaguzi wa Zanzibar kutopatiwa ufumbuzi, Balozi Sefue alisema hakuna hofu yoyote (ya kukosa fedha) kwa sababu tayari kuna hatua kadhaa zimechukuliwa na Serikali ya Tanzania kushughulikia mambo yaliyohojiwa na MCC.

Akieleza zaidi, Balozi Sefue alisema taarifa ya MCC haikusema masuala hayo mawili yaishe vipi, bali walieleza yashughulikiwe; na kwamba hivi sasa yanaendelea kushughulikiwa na yanaendelea vizuri.

Alisisitiza kuwa Tanzania imefuata mashariti yote ya kupata fedha hizo kutoka MCC.

“MCC walituambia sisi kama serikali kuwa yaangalieni masuala haya, na siyo kwamba walituambia tuyashughulikie hadi tuyamalize ndipo watatupatia fedha … hilo siyo kweli,” alisema Balozi Sefue.

Aliongeza kuwa hadi sasa, hatua zilizofikiwa katika kutatua mgogoro wa Zanzibar na pia suala la wahalifu wa makosa ya mtandao, yote hayawezi kuikosesha sifa Tanzania kupata fedha hizo.

MSEMAJI WA SMZ
Msemaji wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, ambaye pia ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mohamed Aboud Mohamed, alikataa kuzungumzia tishio la kukosekana kwa fedha kutoka MCC kwa sababu ya suala la mgogoro wa Zanzibar, kwa maelezo kuwa suala hilo linapaswa kufafanuliwa na Serikali ya Muungano.

Alisema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), haikuandikiwa barua yoyote na MCC na hivyo (wao) hawawezi kulitolea maelezo.

Kuhusiana na mgogoro wa uchaguzi wa Zanzibar, Mohamed alisema hilo pia siyo jambo linalopaswa kutolewa ufafanuzi na SMZ bali ZEC kwani ndiyo wanaosimamia uchaguzi na kwamba, mwenyekiti wao ndiye aliyetangaza kufutwa kwa uchaguzi uliofanyika Oktoba 25, 2015.

YATAKAYOJADILIWA NA BODI MCC
Baadhi ya mada zitakazojadiliwa katika kikao hicho ni pamoja na kupitia adidu za rejea za kikao kilichofanyika Septemba 17, 2015, Mazungumzo kuhusu uchaguzi wa miradi ya kutekeleza kwa mwaka 2016, pamoja na Haki za kidemokrasia nchini Morocco.

Ajenda nyingine ni mazungumzo kuhusu miradi muhimu ya utekelezaji, Kamati ya Ukaguzi kuwasilisha ripoti, kupitisha na kuzijadili nchi wanachama wa MCC zitakazopokea misaada.

Tofauti na fedha zinazotolewa na wafadhili wengi duniani, fedha za MCC hazitakiwi kurudishwa na nchi inayopewa fedha hizo na pia nchi husika hupewa uhuru wa kuchagua aina ya miradi ya maendeleo ambayo inataka igharimiwe na fedha hizo.

Katika fedha za awamu ya kwanza za MCC, Tanzania ilipata dola za Marekani milioni 698 (Sh.trilioni 1.46), ambazo tayari zimesaidia kufanikisha miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwamo ya barabara na usambazaji wa umeme vijijini.
CHANZO: NIPASHE

No comments: