Thursday 23 July 2015

Mgombea Urais Ukawa kupatikana karibuni

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimebuni mbinu mpya ya kudhibiti mamluki wanaochukua fomu za kugombea kupitia chama hicho kisha kutokomea nazo mitini.
Sasa watakaopitishwa na kupewa fomu za chama hicho kugombea ubunge au udiwani, watatakiwa kusaini fomu maalumu mbele ya mahakama ili wakitokomea bila kurejesha fomu Tume ya Uchaguzi (NEC), wapandishwe mahakamani.Kauli hiyo imetolewa leo na Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Willbrod Slaa kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Viwanja vya Magomeni, Jijini Mwanza. “Mwaka huu hakuna kupita bila kupingwa, wagombea wetu wote tutawasainisha mahakamani na wakishindwa kurudisha fomu, tutawashughulikia mahakamani,” amesema Dk. Slaa na kuongeza;  “Waliochukua fomu hatutaki kesho mmoja amejitoa, kama unataka kujitoa ondoka leo, ruksa.”

Mkutano huo umehudhuriwa na wabunge na viongozi mbalimbali wa chama hicho akiwemo Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA Zanzibar, Salum Mwalimu, Naibu Katibu Mkuu Bara, John Mnyika, Makamu Mwenyekiti Bara, Prof. Abdallah Safari; Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake CHADEMA (BAWACHA), Halima Mdee.  Katika mkutano huo, wanachama wapya kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM) walitambulishwa, wanachama hao ni James Lembeli aliyekuwa Mbunge wa Kahama Mjini na Ester Bulaya ambaye alikuwa Mbunge Viti Maalum kutoka Mkoa wa Mara.

Kwenye mkutano huo Dk. Slaa amesema, sasa hivi CHADEMA ipo sehemu yote ya nchi hivyo hakuna mahali ambapo chama hicho kitashindwa kusimamisha mgombea na kwamba, Ijumaa wiki hii watamaliza uteuzi kwenye majimbo yote Tanzania.  “Leo tumeingia kila kona ya nchi, uchaguzi uliofanyika wiki hii ni wa Tanzania nzima, hakuna mahali ambapo CHADEMA haipo tena, hatuzungumzi kabila, hatuzungumzi Magufuli ni mkabila, sehemu zote tunazungumza Utanzania,” anasema Dk. Slaa. Akizungumzia mahudhurio ya wananchi kwenye mkutano huo Dk. Slaa amesema, miongoni mwa waliohudhuria mkutano huo hakuna aliyelipwa fedha wala kubebwa na magari kutolewa kule alikokuwa.


“Hakuna aliyebebwa, hakuna aliyelipwa pesa, mmekuja hapa kwa miguu yenu tangu asububi, asanteni sana na Mungu awabariki,” amesema Dk. Slaa. Hata hivyo amesema, ukiumwa na nyoka hata utapoguswa na jani utalikimbia. Aliwafikirisha wananchi kwa kujiuliza, katika miaka 10 iliyopita, Watanzania walikuwa wanakunywa chai huku sukari ikiuzwa Sh. 500, je leo nani anaweza kunywa chai kwa sukari bei hiyo?

Pia aliwakumbusha kuwa, miaka 10 iliyopita ikiwemo wafugaji waliweza kula nyama, leo bado wanaweza kula kula kilo ya nyama? Dk. Slaa amesema, mwaka 2005 wakati Rais Jakaya Kikwete akiwa mgombea urais kupitia CCM, aliwaahidi Watanzania Maisha Bora kwa Kila Mtanzania lakini sasa maisha yamekuwa magumu kwa kila Mtanzania.

Hata hivyo amesemea, mgomea wa CCM ni mzaliwa wa ukoo ule ule na kabila la CCM hivyo kuna kila sababu ya kuwaonda. Pia amesema, “tumekuja leo ili tuwaeleze kwamba CHADEMA tupo makini, kazi za chama hazisimami, tupo kwenye utekelezaji wa kazi za chama. Hata hivyo, amewaahidi wananchi kuwa, wakati utakapofika “tutadondosha nondo zetu.”

Dk. Slaa amewahahakikishia wananchi kuwa, chama hicho hakiwezi kumeguka wala kusambaratika licha ya kuwepo kwa taarifa kwamba, yeye na Freeman Mbowe ambaye ni mwenyekiti wa chama hicho hawasalimiani, Kwa kujiamini kiongozi huyo amesema, wamejihakikishai kushika dola, “haya sio maneno wala utani.” Msukumo mkubwa wa maisha Dk. Slaa amesema unatokana na mabadiliko ya uchumi ulio mbovu kwa miaka zaidi ya 50 baadaya Uhuru uliopatikana mwaka 1961.

Amefafanua kuwa, wakati wa Rais wa Kwanza, Mwalimu Julius Nyerere, uamuzi ulianza matawini kwenda juu lakini sasa CCM imebadilisha na kuwa uamuzi wa kundi la watu wachache dhidi ya wananchi walio wengi.

“La kwanza tunalolisimamia ni nchi irudi kwa wananchi, ukifanya hivyo yote yanaondoka; ufusadi, wizi rasilimali vyote vitakoma.

“Mkikabidhi nchi kwa wachache hiki ndicho kinatokea, mwaka 2015 ndio mwisho. Katiba inasema serikali itapata madaraka yake kutoka kwa wananchi, CCM imepoka,” amesema.

Akizungumzia ukombozi Dk. Slaa amesema, nchi inahitaji ukombozi na wananchi wapo tayari katika ukombozi na kuwa, Polisi, Wanajeshi na wengine ni watiifu na ndio maana wanawapenda na wanaungana nao katika safari ya ukombozi ambapo vyombo hivyo vitaendelea kuwepo, hofu kuwa upinzani unaleta vurugu haipo tena.

Katika mkutano huo, Mbowe amewatoa hofu wananchi kwamba, Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) uko imara, hadi atakapopatikana rais.

Aidha, Mbowe alianza hotuba yake fupi baada ya kuwakabidhi kadi za uanachana Bulaya na Lembeli.

“Hamtakiwi kuendelea kusikiliza maneno ya uzushi ambayo yanasemwa UKAWA umevunjika au kusambaratika, hayo sio kweli na kuhakikishieni hilo, hadi leo asubuhi nimewasiliana na viongozi wezetu wa UKAWA.”

Amesisitiza kuwa, wananchi hawatakiwi kusikiliza maneno ya nje bali wawasikilize viongozi wao, kwani umoja wao bado unalengo lile lile la kuiondoa CCM madaraka.

Amesema, UKAWA bado wanaendelea na mazungumzo ya amani na kwamba, bado wanamalizia mambao madogo ili wote waende sawa na kutoka na mgombea mmoja “Agosti 4 mwaka huu tutatoa taarifa ya nani rais.”

Hata hivyo amesema, jambo la kwanza ambalo UKAWA italishughulikia ni kurudisha viwanja vyote ambavyo ni mali ya wananchi na sasa vipo chini ya CCM.

Lakini pia amepiga marufuku mausula ya ukabila na kushangazwa katika Karne hii ya 21 kuwepo wapo kwa watu wanaozungumzia ukabila.

Akizungumzia ukabila, alijaribu kuiga sauti ya Mwl. Nyerere ambaye katika hotuba zake alizokuwa akizungumzia ubaya wa kuubeba ukabila katika nchi hii.

No comments: